Wamiliki wa matatu waondoa mgomo wiki ijayo baada ya kuingizwa boksi na Ruto
Wadau wa sekta ya uchukuzi wamefuta mgomo wao walioahirisha Jumanne uliopangwa kufanyika wiki ijayo kulalamikia kupanda kwa bei ya mafuta, kufuatia mazungumzo na Rais William Ruto katika Ikulu ya Mombasa.
Akizungumza Ijumaa, katika Ikulu ya Mombasa, mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Matatu, Albert Karakacha, alisema kuwa wadau wa sekta ya usafiri wamekubaliana kutoendelea na mgomo huo.
“Tumefuta mgomo. Tulikuwa tumeusitisha, lakini sasa tumeufuta kabisa, kwa hivyo hatutakuwa na mgomo wiki ijayo. Tutafanya kazi,” alisema Karakacha, akiongeza kuwa wataendelea kushirikiana na serikali kwa muda wa wiki moja ili kuruhusu mashauriano yanayolenga kutatua mzozo kuhusu kupanda kwa gharama za mafuta, ambayo imechangia kupanda kwa nauli na gharama ya maisha kote nchini.
Bw Karakacha alisema sekta ya uchukuzi itafanya kazi kwa karibu na serikali kushughulikia changamoto zinazohusu bei ya mafuta na matatizo yanayowakabili wamiliki wa matatu.
Mgomo huo ulitatiza huduma za usafiri katika maeneo kadhaa nchini mapema wiki hii, ambapo abiria walikwama baada ya madereva wa matatu na mabasi kusimamisha magari kulalamikia bei ya juu ya dizeli.
Maandamano hayo yalilemaza usafiri Nairobi na miji mingine mikubwa, na kuwaacha maelfu ya abiria wakiwa wamekwama, huku wengine wakilazimika kutembea umbali mrefu kwenda kazini na shuleni.