Kuwait yapiga marufuku wafanyakazi wa nyumbani kutoka Kenya
KUWAIT imepiga marufuku uajiri wa wafanyakazi wa nyumbani kutoka Kenya hatua inayojiri muda mfupi baada ya mageuzi ya ajira nchini Saudi Arabia kusababisha kupungua kwa fedha zinazotumwa nyumbani na Wakenya wanaofanya kazi humo.
Uamuzi huo unaongeza changamoto kwa mkakati wa Kenya wa kusafirisha wafanyakazi nje ya nchi, ambao umekuwa ukitegemewa kushughulikia suala la ukosefu wa ajira na kuongeza mapato ya fedha za kigeni kupitia fedha zinazotumwa nchini na wananchi wanaofanya kazi ughaibuni.
Chini ya kanuni mpya, Wizara ya Masuala ya Ndani ya Kuwait imezuia uajiri wa wafanyakazi wa nyumbani kutoka nchi 27, ikiruhusu uajiri kutoka nchi 10 pekee.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari, hatua hiyo ilifikiwa baada ya mashauriano kati ya Wizara ya Masuala ya Kigeni, Wizara ya Afya na Mamlaka ya Umma ya Wafanyakazi.
Nchi zitakazoruhusiwa kupeleka wafanyakazi wa nyumbani nchini humo ni pamoja na Afrika Kusini, Benin, Eritrea, Ethiopia, Ufilipino, Sri Lanka, India, Vietnam, Nepal na Senegal.
Kenya imejumuishwa pamoja na Uganda, Nigeria, Rwanda, Burundi, Malawi, Cameroon na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo miongoni mwa nchi zilizowekewa vikwazo hivyo.
Hatua hiyo imezua wasiwasi kuhusu mustakabali wa ajira za Wakenya katika nchi za Ghuba wakati ambapo mapato kutoka baadhi ya nchi za Mashariki ya Kati tayari yameanza kudorora.
Saudi Arabia, ambayo kwa miaka ya hivi karibuni imekuwa moja ya vyanzo muhimu vya fedha za kigeni kwa Kenya, imeshuhudia kushuka kwa kiwango kikubwa kwa fedha hizo baada ya kuanzisha mfumo mpya wa vibali vya kazi unaozingatia kiwango cha ujuzi wa mfanyakazi.
Takwimu za Benki Kuu ya Kenya zinaonyesha kuwa fedha zilizotumwa kutoka Saudi Arabia zilishuka mwaka huu kwa asilimia 52.38.
Gavana wa Benki Kuu ya Kenya, Kamau Thugge, amesema mageuzi hayo ya ajira yalivuruga mchakato wa kuajiri wafanyakazi wapya, mikataba ya kazi na mapato ya maelfu ya wafanyakazi wa kigeni wanaofanya kazi za nyumbani, usafi, ukarimu na ulinzi.
Kwa miaka mingi, nchi za Ghuba zimekuwa sehemu muhimu ya mkakati wa kusafirisha wafanyakazi, huku maelfu ya Wakenya wakipelekwa kufanya kazi za nyumbani, usafi, ukarimu na huduma nyingine zisizohitaji ujuzi mkubwa.
Ajira hizi zimekuwa chanzo muhimu cha fedha zinazosaidia familia nyingi kugharamia elimu, huduma za afya na miradi ya maendeleo.
Hata hivyo, sekta hiyo imeendelea kukumbwa na changamoto kama unyanyasaji wa wafanyakazi, ucheleweshaji wa mishahara na ukiukaji wa mikataba.
Kupungua kwa uajiri katika nchi za Ghuba kunatarajiwa kuathiri wafanyakazi, familia zinazotegemea fedha hizo na uchumi wa maeneo mengi ya vijijini.
Aidha, hali hiyo inaweza kulazimisha serikali ya Kenya kutafuta masoko mapya ya ajira na kuwekeza zaidi katika kuwaandaa wananchi kupata kazi zinazohitaji ujuzi wa juu katika mataifa mbalimbali duniani.