Siasa

Tunataka PAWA: Oburu asema anan’gan’gana kutoshea katika viatu vya Raila

Na MOSES NYAMORI March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM), Oburu Oginga, ameanzisha kituo kipya cha shughuli za kisiasa jijini Nairobi huku akiendelea kuimarisha mamlaka yake katika uongozi wa chama hicho kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Ofisi hizo mpya za kibinafsi zilizoko katika eneo la Riverside Drive zimekuwa kitovu cha mikutano na shughuli nyingi za kisiasa, zikifanana na ofisi za zamani za Raila Odinga zilizokuwa katika eneo la Capitol Hill.
Hatua hiyo inajiri wakati Dkt Oginga amechukua usukani wa chama kuelekea makubaliano ya kuunda muungano na chama cha United Democratic Alliance (UDA) kinachoongozwa na Rais William Ruto.
Ofisi hizo zilizinduliwa rasmi Jumatatu, Machi 9, 2026, katika hafla iliyohudhuriwa na viongozi kadhaa wa kisiasa akiwemo Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja. Tangu wakati huo, Seneta huyo wa Siaya ameonekana kufaidika na ushawishi mkubwa ndani ya serikali ya Rais Ruto.
Katika siku tatu zilizopita, Dkt Oginga amefanya mikutano kadhaa muhimu katika ofisi hiyo mpya na viongozi kama Gavana Sakaja, Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi, Gavana wa Migori Ochilo Ayacko na Mwakilishi wa Wanawake wa Nairobi Esther Passaris.
Majadiliano yao yalihusu mipango ya uchaguzi wa 2027, mazungumzo ya muungano wa kabla ya uchaguzi kati ya ODM na UDA, mkutano wa kitaifa wa wajumbe wa chama hicho unaotarajiwa kufanyika Machi 27, pamoja na mikakati ya kuimarisha mtandao wa chama mashinani.
Aidha, Dkt Oginga ameongezewa ulinzi na kupewa gari la usalama linaloandamana na msafara wake. Pia ameruhusiwa kutumia helikopta katika baadhi ya shughuli zake, ikiwemo kuandamana na Rais katika hafla mbalimbali za kisiasa.
Ijumaa iliyopita alihudhuria hafla ya Ramadan katika Ikulu ya Mombasa pamoja na Rais Ruto kushiriki chakula cha Iftar, kufuturu baada ya kufunga mchana.
Vyanzo vya ndani ya chama vinasema ofisi hiyo mpya ilinunuliwa ili kumpa Dkt Oginga mazingira mazuri ya kufanya kazi bila kuingiliwa kisiasa. Hapo awali alikuwa akifanya kazi kutoka ofisi ndogo katika Bunge Towers na makao makuu ya chama ya Orange House.
Awali akionekana kama mwanasiasa aliyefanya kazi kwa utulivu nyuma ya pazia wakati wa uongozi wa ndugu yake Raila Odinga, sasa Seneta huyo ameibuka kuwa mhimili mkuu wa uongozi wa ODM katika kipindi nyeti tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2005.
Mojawapo ya majukumu yake makubwa ni kulinda mpango wa serikali jumuishi kati ya ODM na UDA ulioanzishwa miezi kadhaa kabla ya kifo cha Raila Odinga.
Katika wadhifa wake wa sasa, Dkt Oginga ameibuka kuwa kiungo muhimu kati ya ODM na serikali ya Kenya Kwanza, jukumu linalohitaji busara, uvumilivu na mikakati ya kisiasa.
Hata hivyo, wakosoaji wa serikali jumuishi wanasema hatua ya kumpa Dkt Oginga hadhi na rasilimali zaidi ni mkakati wa kisiasa wa Rais Ruto kuimarisha ushawishi wake ndani ya ODM.