Wanga: ODM haitatoa tikiti ya moja kwa moja 2027, kila mtu ajipiganie
KAMA njia ya kuzuia wanasiasa kuhama na kudumisha ushawishi wake eneo la Nyanza, chama cha ODM kimewahakikishia wafuasi wake kuwa kutakuwa na mchujo huru katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Viongozi wa ODM sasa wanakanusha kuwa baadhi ya wagombea watapewa vyeti vya moja kwa moja jinsi ambavyo imekuwa katika chaguzi za nyuma na kuzua malalamishi mengi.
Mwenyekiti wa ODM, Gladys Wanga, amewaonya wanasiasa kutoka Nyanza dhidi ya kuwahadaa wapigakura kwamba kuna wagombea ambao watapewa tikiti ya moja kwa moja.
“Msikubali mtu yeyote awaambie kwamba yuko karibu na mimi au kiongozi wa chama Dkt Oburu Oginga, na atapewa cheti cha ODM moja kwa moja. Yeyote anayetaka kugombea kwa tikiti ya ODM lazima asake uungwaji mkono kutoka kwa raia,” akasema Bi Wanga.
Kwenye chaguzi za nyuma, ODM kilitoa tikiti ya moja kwa moja na pia kikatumia maelewano ya wagombea kuafikia waliokuwa wakigombea viti mbalimbali.
Baadhi ya wagombea ambao hawakukubali mbinu hizi walijiondoa na kuwania kibinafsi.
Aidha michujo ya ODM nayo imekuwa ikijaa ghasia.
Mnamo 2022 katika Kaunti ya Homa Bay wagombea sita kati ya wanane wa ubunge walipewa tikiti ya moja kwa moja huku wawili wakipitishwa kwenye mchujo.
Bi Wanga alikuwa kati ya walionufaika baada ya kupewa tikiti ya moja kwa moja.
Waziri wa Fedha John Mbadi alijiondoa kwenye kinyángányiro cha ugavana naye marehemu Raila Odinga akamshawishi aliyekuwa Mbunge wa Kasipul Oyugi Magwanga awe naibu wa Bi Wanga.
Safari hii, hata hivyo, ODM inachukua mkondo tofauti, Bi Wanga akisema watatumia mchujo badala ya maelewano ili raia wawe na usemi kuhusu viongozi wao.
“Chama kitafanya uteuzi wa haki na kutoa nafasi sawa kwa kila mgombea. Ni wananchi watakaoamua nani atapeperusha bendera ya ODM kwenye viti vyote vinavyowaniwa,” akasema gavana huyo wa Homa Bay.
Marehemu Bw Odinga ndiye alikuwa akituliza migogoro kuhusu uteuzi wa chama na baada ya mauti yake inaonekana ODM itakuwa na wakati mgumu kuamua nani wa kumpokeza tikiti au kumnyima.
Bi Wanga hata hivyo, anasisitiza kuwa wana kibarua cha kulinda ngome za ODM hata kama Raila hayuko.
“Kulinda chama chetu ni kipaumbele na lazima tushinde viti vingi zaidi katika uchaguzi mkuu ujao ili kuongeza nguvu yetu katika mazungumzo ya kitaifa. Bila uwakilishi wa kutosha, tunaweza kutengwa katika maamuzi muhimu,” akasema Bi Wanga.
Mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma alisisitiza kuwa ODM lazima itengewe ngome zake akiwataka wanasiasa wa UDA kuhamia chama hicho cha chungwa.
“Tunakusudia kufanya uteuzi wa haki na wagombea wote wanapaswa kujiunga na ODM kwa sababu ndiyo ina nguvu eneo hili,” akasema Bw Kaluma.