Tahariri

TAHARIRI: Nani aliyelala kazini shuleni Utumishi Girls?

Na MHARIRI MKUU May 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAIFA la Kenya kwa mara nyingine linaomboleza baada ya mkasa wa kutisha wa moto katika Shule ya Upili ya Utumishi Girls Academy, Gilgil, Nakuru kuua wanafunzi 16 huku wengine wapatao 79 wakijeruhiwa.

Ni tukio la kuhuzunisha linalofufua majeraha ya visa vingi vya moto vilivyowahi kukumba shule nchini miaka iliyopita.

Cha kusikitisha zaidi ni kwamba mkasa huu unatokea chini ya miaka miwili baada ya wanafunzi 21 kupoteza maisha katika moto wa shule ya Endarasha Academy mwaka wa 2024.

Kwa miongo kadhaa sasa, Kenya imekuwa ikishuhudia mzunguko ule ule wa simanzi, hasira, ahadi na baadaye kusahaulika.

Mwaka wa 2001, wanafunzi 67 waliangamia katika Shule ya Kyanguli Boys.

Kabla ya hapo mnamo 1997, wanafunzi 26 walifariki katika shule ya Bombolulu Girls, Kwale, ambayo baadaye ilipewa jina la Mazeras Memorial.

Mwaka wa 1991, wanafunzi 19 waliuawa katika mkasa wa St Kizito Secondary, Meru.

Wengine wanane walikufa shuleni Asumbi Girls, Homa Bay (2012) huku wanafunzi wawili wakiteketea katika Endarasha Boys mwaka wa 2010.

Mbali na visa hivyo vya vifo, moto umekuwa ukiripotiwa mara kwa mara katika shule nyingi nchini.

Ni jambo la kusikitisha kuwa licha ya historia hii ya maafa, hatua madhubuti bado hazijachukuliwa kuhakikisha wanafunzi wako salama.

Mara nyingi, uchunguzi umeonyesha kuwa visa vingi vya moto hutokana na malalamishi ya wanafunzi ambayo hayashughulikiwi ipasavyo na usimamizi wa shule.

Wanafunzi wanapohisi kusikilizwa ni vigumu wao kufikia hatua za hasira na uharibifu.

Hii inaonyesha kuwa suala hili si la miundomsingi pekee, bali pia ni la uongozi na mawasiliano ndani ya shule.

Baada ya visa vya awali, Wizara ya Elimu iliweka sheria kali za ujenzi wa mabweni, ikikataza matumizi ya madirisha ya chuma ambayo huwazuia wanafunzi kutoroka wakati wa dharura.

Hata hivyo, baadhi ya shule zimeendelea kupuuza masharti hayo bila hatua kali kuchukuliwa.

Hili ni jambo lisilokubalika. Sheria zisizotekelezwa hubaki maandishi matupu yasiyo na maana yoyote kwa maisha ya wananchi.

Wakati umefika kwa serikali kuchukua hatua kali dhidi ya shule zinazokiuka viwango vya usalama.

Maafisa wa elimu wanaopuuza ukaguzi wa shule wanapaswa kuwajibishwa.

Aidha, sharti shule ziwe na njia za kutosha za dharura, vifaa vya kuzima moto na mafunzo ya mara kwa mara kwa wanafunzi na walimu kuhusu jinsi ya kukabiliana na majanga.

Hata ingawa baadhi ya visa hivi hutokana na ukosefu wa nidhamu miongoni mwa wanafunzi wenyewe, ni muhimu kuweka mikakati ya kuepusha vifo vinavyoepukika.

Vijana wengi wanaochukua hatua za uharibifu huwa wanajaribu kuwasilisha ujumbe ambao hawajapewa nafasi ya kuutoa kwa njia nyingine.

Mfumo wa elimu usiojali sauti ya wanafunzi unaweza kugeuka kuwa chanzo cha maafa.

Kila mara taifa linapoomboleza watoto waliopoteza maisha katika moto wa shule, viongozi huahidi mabadiliko makubwa.

Lakini baada ya muda, ahadi hizo hupotea pamoja na kumbukumbu za waliokufa.

Kenya haifai kuendelea kuhesabu maiti za wanafunzi kila baada ya miaka michache bila kujifunza.

Usalama wa watoto wetu lazima uwe kipaumbele cha kweli, si kauli za maombolezo pekee.