Habari za Kaunti

Meru kuanzisha doria za kulinda transfoma usiku

Na DAVID MUCHUI June 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAKAZI wa kijiji cha Kithigachio katika eneo la Imenti ya kati, Kaunti ya Meru, wameanzisha doria za usiku ili kulinda transfoma na miundombinu ya umeme dhidi ya uharibifu unaofanywa na wahalifu.

Kwa muda wa miezi mitano, wanaume wa kijiji hicho wameunda kikundi cha ulinzi cha jamii kinachoitwa“Linda Transformer Initiative”, ambapo hujipanga katika vikundi vidogo vya watu watano na kufanya ufuatiliaji wa usiku kucha ili kuzuia vitendo vya uhalifu.

Hatua hiyo ilichukuliwa baada ya ongezeko la visa vya uharibifu wa vifaa vya umeme, ambavyo vimesababisha maeneo mengi kubaki bila umeme kwa muda mrefu.

Kwa mujibu wa wakazi, maeneo jirani pia yameathirika na uharibifu wa transfoma, hali iliyowalazimu kuungana ili kulinda miundombinu hiyo muhimu.

Mpango huo unaungwa mkono na ofisi ya Kampuni ya Umeme ya Meru kwa kushirikiana na jamii, ili kukabiliana na wizi wa mafuta ya transfoma na nyaya za shaba unaosababisha hasara kubwa

Takriban wateja zaidi ya 2,000 wameathirika kutokana na makundi ya wahalifu kulenga transfoma katika maeneo mbalimbali ya Meru.

Katika tukio moja, watu wanane walikamatwa wakiwa wanajaribu kuiba transfoma katika kiwanda cha kahawa cha Munithu.

Mamlaka zinasema uharibifu wa transfoma si tu uhalifu wa kawaida, bali ni tishio kwa uchumi, usalama wa umma na huduma muhimu, huku hasara kubwa ya mamilioni ya shilingi ikiwa tayari imetokea.