• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Jombi aomba kanisa limsaidie kutimua mke

Jombi aomba kanisa limsaidie kutimua mke

Na TOBBBIE WEKESA

KABARI, KIRINYAGA

Kalameni mmoja aliwashangaza waumini wa kainsa moja la hapa alipoingia kanisani na kuomba asaidiwe kumtaliki mke wake akidai alikuwa amegeuka kisirani.

Kulingana na mdokezi, polo alikuwa amechoshwa na tabia za mkewe za kumzomea kila mara. Inadaiwa polo alikuwa amejaribu mbinu zote za kumtimua kipusa lakini hakufua dafu.

Duru zinasema kipusa alipokuwa akienda kanisani, polo aliamua kumfuata polepole. Wakati mahubiri yalipoanza, polo aliingia na kumuomba pasta atulie kidogo.

“Mke wangu hushiriki hapa. Nyumbani hanipi amani wala raha. Niliamua kuzamia pombe angalau nisahau baadhi ya mambo anayonifanyia,” polo alieleza. Kila mtu kanisani alinyamaza kimya kumsikiliza polo.

“Najuta sana kumuoa. Nimejaribu kumfukuza lakini hafukuziki. Naomba talaka,” polo alisema. Mkewe polo alisimama na kumuomba pasta kutomsikiliza mumewe.

“Achana na huyo. Ni mlevi. Wewe endelea na mahubiri,” kipusa alimrai pasta.Inasemekana polo alianza kumzomea kipusa huku akitoboa siri zake zote.

“Acha ujinga. Huyu mwanamke kitandani hatuangaliani. Akiondoka asubuhi yeye hurudi jioni na hataki nimuulize. Mnisaidie nimpe talaka,” polo aliomba. Kulingana na mdokezi, pasta alimuomba polo kurudi nyumbani ili wasuluhishe mgogoro baadaye.

“Tutakuja kusuluhisha hayo mambo baada ya huduma kuisha. Tulia pale kwanza,” pasta alimrai polo. Inadaiwa polo aliamua kuondoka huku akiapa kutumia mbinu zote kumtimua kipusa.

“Sitaki kumuona kwangu. Madharau yake yamenifika kooni. Atafute bwana mwingine wa kumuoa humu kanisani,” polo alisema huku akianza safari kurudi kwake.

Baada ya ibada pasta alielekea kwa jamaa akiandamana na wazee kadhaa na haikujulikana ikiwa walifaulu kusuluhisha mzozo kati yake na mkewe

You can share this post!

Hazard nguzo tegemeo na mhimili tosha wa Chelsea

Kayole Asubuhi waondolewa Super 8

adminleo