Habari za Kitaifa

Naam, napenda vitu vya bei ghali na huu ndio udhaifu wangu, akiri Murkomen


SIKU mbili baada ya kutaka kuandaliwe Mswada wa Ukaguzi wa Mitindo ya Maisha kwa watumishi wa umma, Waziri wa Barabara na Uchukuzi Kipchumba Murkomen amejibu maswali mengi yaliyoulizwa na Wakenya kuhusu maisha yake ya kifahari.

Seneta huyo wa zamani wa Elgeyo Marakwet na Kiongozi wa Wengi katika Seneti alifichua anapenda mavazi ghali, nguo na vitu vingine vya kifahari, akisema kuwa kushikilia ofisi ya umma hakuhitaji mtu kuwa fisadi ili kumudu vitu hivyo.

Katika ufichuzi wake wa moja kwa moja kwenye Obina TV,  Murkomen alikiri kumiliki saa ya Rolex yenye thamani ya Sh900,000, jozi ya viatu vya Sh80,000, mshipi wa Sh50,000, tai ya Sh20,000 na suti ya Sh30,000.

Alisema hivi majuzi amevalia mavazi ya zamani ya Casio G-Shock yenye thamani ya Sh9,000, ambayo kwa sasa inauzwa kwa Sh13,000 sokoni.

“Nina saa (Rolex) iliyonigharimu Sh900,000, hii niliyovaa ni Casio G-shock ambayo niliinunua kwa Sh9,000 lakini imetajwa na wale wa mitandao ya kijamii kuwa ya Sh400,000,” Bw Murkomen alisema katika mahojiano Jumatatu usiku katika Obina Show.

Mwanasiasa huyo alisema kutokana na chuki kwenye mitandao ya kijamii ameacha kutumia saa ya bei ghali ili asichunguzwe zaidi.

“Baadhi ya mavazi ni ghali kupata kwa sababu ni ya kudumu na yanaweza kudumu kwa miaka 20 bila kupoteza thamani. Kama saa yangu, nasikia thamani yake itaongezeka na huenda nikaiuza kwa faida katika siku zijazo,” alieleza.

“Kila binadamu ana kitu kimoja ambacho kinamgeuza kutumia rasilimali ambazo zilikusudiwa kwa ajili ya kitu kingine, kitu ambacho kinaweza kuwa cha thamani zaidi. Hapo ndipo udhaifu wangu ulipo lakini niko tayari kurekebisha njia zangu,” aliendelea.

Aliongeza, “Ninapoenda kwenye maduka ya rejareja na mke wangu na watoto, wanatamani kuniondoa kwenye sehemu ya viatu kwani nitaishia kuvinunua.”

Waziri huyo alidai kuwa mapenzi yake katika saa yalianza akiwa shule ya msingi na alivalia moja aliyonunuliwa na babake mwaka wa 1991 alipokuwa darasa la sita, kama shukrani kwa kupata alama bora zaidi katika darasa lake.

Murkomen alisimulia jinsi babake alivyomchochea kufaulu shuleni kwa kuahidi saa ikiwa angeongoza darasa lake, jambo ambalo lilimchochea kupendezwa na saa maisha yake yote.

Alisema madai kwamba anaringa na ni mfisadi ni ya uongo yanayoenezwa na wanaomchukia kwa kuwa wazi na kutokubali rushwa.