Habari za Kitaifa

Kandie tegemeo Berlin Marathon Jumapili kampuni ya NMG ikiandaa onyesho bomba Eldoret

Na GEOFFREY ANENE September 28th, 2024 1 min read

ZAIDI ya washiriki 80,000 kutoka mataifa 150 wakiwemo 58,212 katika kitengo wazi watatimka kwenye makala ya 50 ya mbio za Berlin Marathon nchini Ujerumani, leo.

Bingwa wa zamani wa Berlin Marathon, Paul Tergat amemiminia sifa mshikilizi wa zamani wa rekodi ya dunia ya 21km, Kibiwott Kandie akisema ana uwezo pia wa kung’aa katika 42km.

“Namfahamu vyema Kandie. Ana uwezo mkubwa na pia bado ana umri mdogo. Barabara mjini Berlin ni tambarare kwa hivyo muda ya kasi ya juu unaweza kupatikana hapa,” akasema Tergat akaambia vyombo vya habari nchini Ujerumani.

Kandie anatarajiwa kupata ushindani mkali kutoka kwa Muethiopia Tadese Takele bila kusahau wapinzani wengine wakiwemo Wakenya Samwel Mailu, Stephen Kiprop, Cybrian Kotut, Philimon Kipchumba, Josphat Boit, Enock Onchari, Justus Kangogo na Asbel Rutto hawawezi kupuuzwa.

Veronica Maina na Pauline Esikon ni Wakenya pekee katika kitengo cha wanawake.

Mbio za Berlin Marathon zitapeperushwa na runinga ya NTV. Shirika la Habari la Nation (NMG) pia limeandalia mashabiki sehemu ya kutazama mbio hizo kwenye runinga kubwa katika barabara ya Uganda Road mjini Eldoret kaunti ya Uasin Gishu.