Walioteuliwa kusimamia IEBC wana uhusiano na Raila na Ruto
WATU watano kati ya saba walioteuliwa na Rais William Ruto kusimamia Uchaguzi Mkuu ujao wana uhusiano wa moja kwa moja au usio wa moja kwa moja naye pamoja na mshirika wake katika serikali Jumuishi, Raila Odinga, hali ambayo imezua malalamishi kutoka kwa upinzani kwamba walioteuliwa hawatakuwa waamuzi huru.
Baadhi yao wamekuwa washirika wao wa kisiasa hapo awali, mmoja akiwa mshauri wa kisheria wa chama cha zamani cha ANC kilichoasisiwa na Mkuu wa Mawaziri, Musalia Mudavadi.
Mnamo Alhamisi Rais alimteua Erastus Edung Ethekon, aliyekuwa wakili wa Kaunti ya Turkana, kuwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC). Pia aliteua Msajili wa Vyama vya Kisiasa Ann Nderitu, Moses Alutalala Mukhwana, Mary Karen Sorobit, Hassan Noor Hassan, Profesa Francis Odhiambo Aduol na Fahima Araphat Abdallah kuwa makamishna.
Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka tayari amemkosoa Rais Ruto akidai upendeleo katika uteuzi huo. “Tuna wasiwasi mkubwa kwamba Bw Ruto alichagua kuwa na upendeleo kwa kupuuza kanuni ya mashauriano na makubaliano katika aliopendekeza kuwa Mwenyekiti na makamishna wa IEBC.
Hatua hii imeunda taasisi isiyoaminika moja kwa moja. Kama tulivyosema katika mawasiliano ya awali kuhusu suala hili, sasa ni dhahiri kuwa nia ni kuiba si tu uchaguzi mkuu ujao bali pia chaguzi ndogo zijazo,” Bw Musyoka alidai, huku akiahidi taarifa ya kina kutoka kwa upinzani Jumatatu.
Bw Ethekon, ambaye anatarajiwa kumrithi Bw Wafula Chebukati ni mshirika wa karibu wa Naibu Mkuu wa Wafanyakazi wa Rais Ruto, Josephat Nanok. Bw Ethekon alihudumu kama Wakili wa Kaunti ya Turkana wakati wa utawala wa Bw Nanok ambaye wakati huo alikuwa Gavana wa Turkana kupitia tiketi ya chama cha ODM cha Bw Odinga.
Dkt Mukhwana, aliyeteuliwa kama kamishna, kwa sasa anahudumu katika jopo la kazi la Rais Ruto la kushughulikia maslahi ya wafanyakazi katika sekta ya afya tangu 2024. Ni mshirika wa karibu wa Bw Mudavadi, ambapo aliwahi kuwa mshauri wake wa kisheria katika chama cha ANC.
Bi Sorobit kutoka Kaunti ya Uasin Gishu pia ni mshirika wa karibu wa Rais Ruto tangu alipokuwa kiongozi wa chama cha URP.
Bi Abdallah ni mshirika wa karibu wa Gavana wa Lamu Issa Timamy. Bw Timamy ni mshirika wa karibu wa Mudavadi ambaye aliwahi kuongoza chama cha ANC kabla ya kuwa naibu kiongozi mwenza wa chama cha UDA.
Bw Hassan Noor Hassan ni mwanachama mwaminifu wa ODM ya Bw Odinga, na aliwania bila mafanikio kiti cha ugavana wa Mandera katika uchaguzi uliopita. Pia anahusishwa na Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed, rafiki wa karibu wa Bw Odinga.
Bi Nderitu, kwa sasa Msajili wa Vyama vya Kisiasa, aliwahi kufanya kazi katika IEBC. Profesa Aduol kutoka Kaunti ya Kisumu ni Makamu Mkuu wa zamani wa Chuo Kikuu cha Ufundi cha Kenya