Habari za Kaunti

Homa Bay yaanza kuvuna hoteli zikijaa kuelekea sherehe za Madaraka

Na GEORGE ODIWUOR May 26th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

WAFANYABIASHARA Homa Bay wanatarajia kuvuna pakubwa huku kaunti hiyo ikiwa mwenyeji wa Sherehe za Madaraka Dei mnamo Juni 1.

Usimamizi wa hoteli kadhaa ulithibitisha kuwa utakuwa makao ya wageni mashuhuri na itakuwa vigumu kupata nafasi ya kuwasitiri watu wengine wa kawaida.

Wikendi, baadhi ya hoteli zilikuwa zimejaa na waliokuwa wakitafuta nafasi waliambiwa wasake makao kwingine. Hoteli ya hadhi ya Cold Spring yenye uwezo wa kuwapa makao wageni 70 tayari imejaa kwa kuwa vyumba vyake vimelipiwa na vitatumika na wageni watakaohudhuria sherehe za Madaraka.

Usimamizi wa Cold Spring uliambia Taifa Leo kwa wateja wao ni maafisa kutoka ubalozi mbalimbali. Meneja wa hoteli hiyo Dickson Osore alisema wageni wengi watawasili hotelini humo Mei 31 kisha kuondoka Juni 1.

Kwa mujibu wa Bw Osore, chumba cha mwisho kililipiwa wiki iliyopita.

“Wengine watakwepo hadi baada ya Juni 1. Lakini kwa sasa vyumba vyote 70 vimelipiwa,” akasema  Bw Osore huku akisema wanalenga kutumia sherehe hizo kuvumisha hoteli yao.

“Sherehe hizi zitakuwa silaha ya kuvumisha hoteli zetu Homa Bay na sekta ya utalii. Huwa tuna huduma bora na tunawaalika wageni wote hata baada ya sherehe za Madaraka,” akaongeza.

Homa Bay pia itakuwa mwenyeji wa Kongamano la Ugatuzi mnamo Agosti mwaka huu, lile la uchumi samawati na Maadhimsho ya Siku ya Chakula Duniani.

Hoteli nyingine ambazo zimejaa Homa Bay ni Golden Ray, Twin Towers na Tausi.