Simu ilivyotibua shambulizi katika KICC na kufanikisha la Dusit

MNAMO Februari 2018, polisi walitibua shambulio kubwa la kigaidi baada ya kuua gaidi mmoja na kuwakamata wengine wawili.
Makabiliano kati ya polisi na wahalifu hao yalitokea katika eneo la Merti, kaunti ya Isiolo ambako maafisa hao wa usalama pia walipata silaha mbalimbali ikiwemo magurunedi 36 na bunduki tano za rashasha.
Gari moja lililobeba vilipuzi pia lilinaswa.
Magaidi walikuwa wamepanga kulipua bomu lililobebwa kwenye gari, katika Jumba la Mikutano ya Kimataifa ya Jomo Kenyatta (KICC) jijini Nairobi.
Washukiwa waliokamatwa walitambuliwa kama; raia wa Somalia Abdimajit Hassan Adan, 24 na Mkenya Mohammed Nane, 23.
Wawili hao walipatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miaka 19 gerezani kwa kupanga shambulio la kigaidi.
Mwaka mmoja baadaye, mnamo Februari 15, 2019, magaidi wenye silaha walivamia Jumba la Kibiashara la DusitD2, lililoko Nairobi na kuwauawa watu 21 huku wengine wengi wakipata majeraha mabaya.
Katika shambulio la DusitD2, washukiwa wawili, Hussein Mohamed Abdille na Mohammed Abdi Ali walifunguliwa mashtaka kortini.
Walikabiliwa na makosa 21 yanayohusiana na ugaidi, kupata vitambulisho vya kitaifa vya Kenya kinyume cha sheria na kufanikisha utekelezaji wa ugaidi.
Sasa uamuzi huo ambao ulitolewa Mei 22, 2025 na Jaji Diana Mochache katika Mahakama ya Kahawa, umefichua uhusiano kati ya kisa cha Merti na shambulio la DusitD2.
Jaji Mochache alisema ushahidi uliowasilishwa na mchunguzi mkuu kutoka makao makuu ya Kikosi cha Polisi Wa Kupambana na Magaidi (ATPU) ulionyesha uhusiano wa visa hivyo viwili.
Bw Titus Lagat, ambaye ni mpelelezi katika ATPU, alifichua kwamba, Hussein Mohamed Abdille alikuwa na uhusiano wa karibu na Abdimajit Hassan, mtuhumiwa katika kisa cha Merti.