Mbunge asifu SHA, Duale akikosoa Raila kuhusu CDF
MBUNGE wa Wajir Kaskazini, Ibrahim Saney, amesema kuwa Bima mpya ya Afya ya Jamii (SHA) imewafaa wakazi wa eneobunge lake kiafya, akisema changamoto zilizoshuhudiwa hapo awali sasa hazipo.
Bw Saney akiongea kwenye mkutano na wakazi wa eneobunge lake aliwataka wananchi wachukulie kwa uzito masuala ya afya na wajisajili kwa SHA. Alitoa mfano wa akina mama na watoto ambao wamenufaika na matibabu kwa kutumia SHA akisema wamelipiwa huduma ambazo walipokezwa.
“SHA japo mwanzoni ilikuwa na changamoto zake, hapa kwetu naona hali imeimarika. Kwa mara ya kwanza wanaougua saratani wanatibiwa huku wanawake wanaojifungua pia wakitumia SHA,” akasema Bw Saney.
Mbunge huyo alimtaka Waziri wa Afya, Aden Duale, ajizatiti na kupambana na wakora ambao wamekuwa wakihujumu mpango wa serikali kuwapa Wakenya huduma bora za kimatibabu.
“Uteuzi wa Duale japo ulionekana kama haukufaa na watu wengine lakini sasa umeanza kuzaa matunda kutokana na jinsi wizara inavyosimamiwa na shughuli kuendeshwa. Duale na Rais Ruto wanastahili kukaza kamba zaidi kuhakikisha huduma bora za afya zinawafikia Wakenya wote,” akaongeza.
Wakati huo huo mbunge huyo ametofautiana na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, akisema Hazina ya Fedha ya Ustawi wa Maeneobunge (CDF) inastahili kusalia mikononi mwa wabunge na si kupokezwa magavana.
“CDF ndio inahusika na maendeleo na wabunge ni rahisi kufikiwa kuliko magavana. Raila akome shinikizo zake na aangazie matunda ya CDF,” akasema.