Siasa

Washirika wa Ruto wavamia ngome ya Kalonzo, Gachagua

Na PIUS MAUNDU June 7th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka na kiongozi wa chama cha Democracy for Citizens Rigathi Gachagua walionyesha ujasiri Ijumaa walipokuwa wakifanya kampeni katika Kaunti ya Makueni, huku Rais William Ruto akiongeza juhudi za kunyakua kura 2 milioni za ngome ya makamu rais wa zamani.

Vinara hao wa upinzani walikosoa mipango ya kuwawezesha wanawake na vijana, ambayo ya washirika wa Rais Ruto walipohutubia mikutano katika miji ya Malili, Salama, Sultan, Emali, Makindu, Kibwezi na Kambu.

Bw Musyoka pia alimlaumu Rais Ruto kwa kutumia urasimu kuzuia upanuzi wa barabara kuu ya Mombasa-Nairobi uliopangwa kufanywa na kampuni ya Amerika huku akiwaita washirika wa Rais katika eneo hilo kuwa wasaliti wanaostahili kuadhibiwa kupitia kura.

Bw Gachagua aliwahimiza wapiga kura wa Ukambani kuwa waangalifu na njama ya Rais Ruto ya kugawanya upinzani.

“Rais Ruto anapaswa kueleza chanzo cha mamilioni ya pesa anazotumia kwa jina la kuwawezesha wanawake. Huu ni ufisadi kwa njia ya mkato. Hizi ni fedha za umma. Chukueni pesa hizo wakizileta,” alisema Bw Musyoka katika Mji wa Malili.

Katika Mji wa Emali, Bw Gachagua aliwataka wapiga kura wa Ukambani kumkataa Rais Ruto na kumuunga mkono Bw Musyoka na washirika wake katika Uchaguzi Mkuu wa 2027, huku akiahidi muungano thabiti wa upinzani.

“Ili Kalonzo afaulu, ni lazima aheshimiwe nyumbani. mkimtaka kiongozi afanikiwe, mpeni wabunge wa kutosha,” alisema aliyekuwa Naibu Rais.

Bw Musyoka alijisawiri kama chaguo bora la upinzani kumpinga Rais Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027, huku washirika wake wakipuuza mivutano ya mamlaka inayoshukiwa kutikisa upinzani.

“Kalonzo si Raila Odinga ambaye kura zake huibwa kirahisi,” alisema.

Gavana wa Makueni Mutula Kilonzo Junior alisema jamii ya Wakamba haiko tayari kumuunga mkono mgombea mwingine yeyote wa urais mwaka 2027 isipokuwa Bw Musyoka.

Ziara hizi za ghafla za vigogo wa upinzani zilifanyika wakati washirika wa Rais Ruto wameongeza juhudi kuvamia Ukambani. Wamekuwa wakizunguka katika eneo hilo kabla ya ziara ya Rais iliyopangwa kufanyika baadaye mwezi huu, wakitoa mamilioni ya pesa katika Kaunti za Kitui, Machakos na Makueni katika harambee za kuwawezesha wanawake na vikundi vya vijana.

Timu ya viongozi mashuhuri ikiongozwa na Spika wa Bunge la Taifa Moses Wetangula ilikuwa katika Migwani, Kaunti ya Kitui na Machakos mjini jana.

Timu ya Bw Wetangula ilisisitiza dhamira ya serikali ya Rais Ruto kutekeleza miradi ya maendeleo na mipango mingine katika maeneo yote ya nchi bila ubaguzi.

Mnamo Alhamisi, timu iliyoongozwa na Naibu Rais Kithure Kindiki ilifanya harambee kusaidia vikundi vya wanawake na vijana katika Mji wa Zombe (Kitui) na Mji wa Mukuyuni (Makueni). Prof Kindiki alisema harambee hizo ni sehemu ya ahadi alizotoa Rais Ruto wakati wa kampeni.

“Wakati Bw Gachagua alikuwa Naibu Rais, aliwahi kushiriki kuchangisha fedha kusaidia wanawake na vijana kama anavyofanya Prof Kindiki? Hakuwa anashughulika na kujitajirisha na kununua hoteli za kifahari?” alihoji Seneta wa Kericho Aaron Cheruiyot katika mji wa Mukuyuni.

Mbali na juhudi za washirika wake, Rais Ruto ameendelea kuwanasa washirika wa Bw Musyoka. Spika wa Kaunti ya Kitui Kelvin Katisya na mwenzake wa Machakos Anne Kiusya wamejiunga na kambi ya Rais Ruto baada ya kumtoroka Bw Musyoka.

Mbunge wa Mavoko Patrick Makau, ambaye ni wa Wiper, amejitokeza wazi kupinga ushirikiano wa Bw Musyoka na Bw Gachagua. Vilevile, Mbunge wa Mwingi Magharibi Charles Nguna ni miongoni mwa washirika wa Bw Musyoka waliotoa dalili za kuungana na Rais Ruto.

“Tunataka siasa za maendeleo, sio maneno matupu,” alisema Bw Nguna alipojiunga na washirika wa Rais Ruto kuendeleza mpango wa uwezeshaji katika Migwani, Kaunti ya Kitui.