Hi cousin? Gachagua anavyofufua siasa za ubinamu nchini
MAPEMA mwezi huu aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alifanya ziara ya kisiasa Ukambani, akitambua jamii ya Wakamba kama “ndugu waliopotea” wa muungano wa GEMA — yaani, Wakikuyu, Waembu na Wameru.
Kwa kuwaita Wakamba “binamu”, Bw Gachagua alijaribu kuandika upya simulizi la kikabila huku akipanua mipaka ya ushawishi wa kisiasa wa Mlima Kenya kuelekea uchaguzi mkuu ambao utakuwa na ushindani mkali dhidi ya Rais William Ruto.
Kauli ya “ sasa binamu” imepanuliwa hadi kwa jamii nyingine za Kibantu, ikigeuka kutoka utani wa kisiasa hadi kuwa mkakati wa kimakusudi wa kuunda miungano ya kisiasa .
Ingawa Rais Ruto amewakosoa hadharani Gachagua na wandani wake kama viongozi wa “siasa za kikabila,” ukosoaji huo pia una mapungufu.
Ruto mwenyewe alipanda ngazi kwa kujenga miungano ya kikabila, hasa kati ya Wakalenjin, Wakikuyu na Waluhya.
Kwa hivyo, siasa za ubinamu zinazoendeshwa na Bw Gachagua si jambo geni, bali ni mwendelezo wa utamaduni wa kisiasa wa Kenya ambapo kabila limekuwa kiini cha mikakati ya uchaguzi.
Lugha ya “ubinamu” huenda ikaleta sura ya umoja, lakini haibadilishi ukweli kwamba mfumo wa siasa za mgawanyiko bado umetawala.
Katika historia ya Kenya, miungano ya kisiasa imejengwa mara kwa mara kwa msingi wa kabila badala ya sera.
Tangu enzi za ukoloni na uhuru, wanasiasa waliunda vyama vya kikabila ili kujihakikishia nafasi katika meza ya maamuzi.
Hii ilijumuisha ushawishi wa vikundi kama Kalenjin Political Alliance, Maasai United Front, na vyama vya pwani kama CAPU chini ya Ronald Ngala. Wengine walikuwa Masinde Muliro aliyeongoza WALU ya Waluhya.Miungano hiyo ilichangia kuundwa kwa KADU — chama kilichokuwa na jamii za walio wachache waliokuwa na hofu ya kutawaliwa na miungano ya Kikuyu na Luo chini ya KANU.
Miaka ya 1970, GEMA (Gikuyu, Embu, Meru Association) ilibuniwa rasmi kama nguzo ya uongozi wa Mzee Jomo Kenyatta, ikilenga kuimarisha ushawishi wa kisiasa wa Mlima Kenya kwa kujumuisha jamii zinazofanana kwa karibu kitamaduni.
Muungano huo uliimarishwa kupitia wanasiasa kama Njenga Karume na Mulu Mutisya walioteuliwa na Rais Kenyatta hadi bungeni, na hivyo kupanua ushawishi wa Mlima Kenya kupitia vyama kama New Akamba Union na Luo Union — ambavyo vilitumika kama majukwaa ya utaifa wa kikabila.
Kwa hivyo, kauli za Gachagua kuhusu ‘ubinamu’ si mpya. Ni mwendelezo wa mbinu ya zamani ya kuunda miungano ya kikabila kwa lengo la uchaguzi.
Kwa sasa, anaelekeza macho yake kwa jamii ya Wakamba — takriban asilimia 11 ya idadi ya Wakenya — ambao mara nyingi wamekuwa upande wa GEMA, isipokuwa mwaka 2007 walipomuunga mkono Kalonzo Musyoka chini ya ODM-K kabla ya kuungana na PNU mwaka wa 2008.
Raila Odinga, kama babake Jaramogi, amekuwa akitegemea kura za jamii ya Luo kwa ushawishi wa kisiasa. ODM ilianza kama jukwaa la upinzani dhidi ya kile kilichotajwa kuwa utawala wa “Mt Kenya mafia.”
Kauli maarufu ya “41 dhidi ya 1” iliunganisha jamii za Luo, Kalenjin na baadhi ya Waluhya dhidi ya PNU ya Kibaki.Leo hii, Rais Ruto, akiwa na uhakika wa uungwaji mkono kutoka kwa Wakalenjin, anakabiliwa na changamoto kutoka kizazi kipya cha wapigakura — maarufu kama Gen Z — wasiofungamana na siasa za kikabila.
Ametafuta ushirikiano na Raila Odinga kama njia ya kuunganisha kura za jamii ya Luo chini ya serikali jumuishi..Wakati huo huo, Gachagua anaendelea na harakati zake za kuunganisha jamii za Kibantu, huku Fred Matiang’i naye akifanya ziara ya kwanza nchini Kisii baada ya kurejea kutoka Amerika— akilenga kuimarisha ushawishi wa jamii ya Kisii (asilimia 6 ya idadi ya Wakenya).
Mkakati huu si mpya. Marais wote wa Kenya — Kenyatta, Moi, Kibaki, Uhuru na sasa Ruto walipata mamlaka kupitia miungano ya kikabila. Vyama vyao havikujengwa juu ya sera, bali ni vyombo vya kupata mamlaka.