Furaha riboribo Kenya Police wakiandikisha historia na kutwaa KPL
Kenya Police Jumapili waliandikisha historia kwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu (KPL) baada ya kuwa ligini kwa misimu minne.
Baada ya kupandishwa KPL mnamo 2021, Kenya Police walishinda ubingwa baada ya kuichapa Shabana 1-0 katika uga wa Kenyatta, mjini Machakos.
Brian Okoth aliwaamsha mashabiki wa Kenya Police baada ya kuruka juu na kufunga mpira wa kichwa mnamo dakika ya 75.
Matokeo hayo yaliwaacha Kenya Police ikiwa na alama 64 na kutamatisha subira ya miaka mitatu ya kutoshinda KPL.
Gor Mahia ambao wamelemewa kutetea ubingwa wao nao walipiga Ulinzi Stars 3-2 kwenye uwanja wa Ulinzi Sports Complex lakini wapo alama sita nyuma ya Kenya Police ikiwa imebakia mechi moja msimu utamatike.
Iwapo Kenya Police wangeshindwa na Gor ishinde, basi mshindi wa KPL angeamuliwa katika mechi ya mwisho Jumapili ijayo wakati ambapo Gor na maafisa hao wa usalama watavaana.
Police walikuwa na mwanzo mbaya wa msimu kwa kuwa baada ya mechi nane, walikuwa wamepata ushindi moja pekee, wakipata sare tano na kupoteza mara mbili. Kipindi hicho walikuwa kwenye eneo hatari la kushushwa ngazi.
Ni matokeo hayo duni ndiyo yalisababisha uongozi wa klabu hiyo kufurusha benchi ya kiufundi ambayo wakati huo ilikuwa ikiongozwa na Salim Babu.
Timu hiyo ilishuhudia mabadiliko baada ya kuteuliwa kwa Etienne Ndayiragije, raia wa Burundi ambaye awali alikuwa ameongoza timu ya taifa ya Tanzania na pia Burundi.
Ni mbinu za ukufunzi za raia huyo wa Burundi ndizo zilisaidia Kenya Police hatimaye kutwaa ubingwa wa KPL. Gor Mahia sasa itaridhika na nafasi ya pili hata ikishinda mechi ya mwisho.
Hata hivyo, KāOgalo wana nafasi ya kuwahi ubingwa wa Mozzart Bet ambako watakutana na Nairobi United inayoshiriki Supa Ligi, kwenye fainali.
Baada ya kushinda taji la KPL, Kenya Police watashiriki Kombe la Klabu Bingwa Afrika (CAF) huku nayo mshindi wa MozzartBet akishiriki Kombe la Mashirikisho Afrika (Caf).