Wasimulia mateso ndani ya seli aliyouawa Ojwang
Kifo cha hivi karibuni kilichofanya kituo cha polisi cha Nairobi Central kumulikwa kimeibua tena kumbukumbu za visa vya mateso ambayo yamekuwa yakifanyika kwenye seli katika kituo hicho.
Albert Omondi Ojwang alifariki akiwa mahabusu baada ya kukamatwa nyumbani kwake Kasipul, Kaunti ya Homabay na maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) waliotumwa kumkamata kufuatia malalamishi yaliyowasilishwa na Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat.
Wale waliowahi kuzuiliwa katika seli hizi walisema mateso waliyopata ndani ya seli hizo yalikuwa mabaya kiasi kwamba hawakutaka hata kufikiria kuendeleza kesi hizo kwa sababu walitoka wakiwa na hofu na mshtuko kutokana na yaliyotokea.
Mwenyekiti wa zamani wa shule ya sheria ya Kenya( KSL), Bw Joshua Okayo, wiki hii aliwaambia waandishi wa habari kwamba Bw Samson Talam, Mkuu wa Kituo (OCS) aliyesimamishwa kazi, alimshambulia kwa nguvu na hata kumvua mavazi yake akayararua vipande vipande.
Bw Talam alikamatwa mwishoni mwa wiki na anatarajiwa kushtakiwa kwa mauaji ya Ojwang, lakini aliambia Mamlaka ya Usimamizi wa Polisi (IPOA), hakuwa kwenye kituo wakati Ojwang alipokufa.
Akizungumza na Taifa Leo , Bw Okayo alisema alikuwa sehemu ya waandamanaji dhidi ya utekaji nyara katika Mtaa wa Aga Khan, Nairobi, Desemba 30 2024 wakati maafisa wa polisi walipomkamata yeye na watu 22 wengine.
“Polisi walitumia nguvu na kutukamata sisi wote 23. Tulipofikishwa kituoni, mambo yalizidi kuwa mabaya baada ya maafisa kujaribu kutugawanya, jambo ambalo tulikataa,” alisema.
Seneta wa Busia, Okiya Omtata, alikuwa miongoni mwa waliokamatwa.
Kwa mujibu wa Bw Okayo, maafisa walitaka kuwatenganisha ili kuwaondoa kwa urahisi.
Waliposhindwa, walimjulisha Bw Talam ambaye alifika seli na maafisa 20.
“Maafisa 20 walibeba fimbo walizotumia kutupiga kwa ukatili huku OCS akichukua jukumu la kunipiga. Alinipigana kwa mikono na hata kurarua fulana yangu vipande vipande,” alisema Bw Okayo.
Alisema Bw Talam alimshambulia kwa takriban dakika 30. Ian Obong’o anakumbuka kila kitu kilichotokea siku hiyo alipokamatwa pamoja na Bw Okayo.
Alisema maandamano hayo yaliyokuwa ya amani yalibadilika kuwa mabaya baada ya polisi kutumia gesi ya kutoa machozi ili kuwatawanya.
“Walitutia mbaroni na kutupeleka kituo cha polisi cha Central. Katika seli walituumiza, jambo lililokiuka sheria kwa sababu tulikataa kutenganishwa,” alisema.
Bw Obong’o alisema askari James Mukhwana aliyekamatwa na IPOA na kushtakiwa kwa mauaji ya Ojwang, alimshambulia binafsi.
Alisema OCS alikuwepo pamoja na maafisa wengine waliotaka kuwadhuru.
“Askari Mukhwana ndiye alikuwa na funguo za seli. Nakumbuka alinipiga mwenyewe baada ya kukamatwa. Walitupiga huku tukikwamolia mnyororo. Ni sheria gani inayomruhusu polisi kumpiga mtu aliye ndani ya seli?” alihoji.
Mnamo Julai 2024, Bw Emmanuel Mokua alikuwa akifanya biashara ya kuuza soseji na mayai karibu na Archives kati kati ya Nairobi wakati alikamatwa na maafisa wa kaunti ya jiji, maarufu kama ‘Kanjo.’
Bw Mokua alidhani maafisa wangeomba hongo kidogo na kuwaachilia, lakini haikufanyika hivyo.
“Badala yake walitutupa kwenye gari la kaunti, walikamata watu zaidi na kutufikisha kituo cha polisi cha Nairobi Central,” alisema.
Alisema usiku huo maafisa walimpiga viboko huku akilala.
Alisema aliteswa vibaya na maafisa wa kaunti walichukua pesa siku iliyofuata na kumwachilia huru.
“Kwa kweli, ningependa kuachana na biashara hii lakini sina budi kuendelea. Kilichotokea usiku huo hakikuwa kizuri,” alisema.