Kimataifa

Makombora ya Iran yaharibu hospitali kubwa zaidi kusini mwa Israel

Na REUTERS June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

TEHRAN, Iran

ISRAEL Alhamisi ilishambulia kituo kimoja kikuu cha mitambo ya kinuklia nchini Iran huku makombora ya Iran yakiharibu Soroka, hospitali kubwa zaidi kusini mwa Israel, vita kati ya nchi hizo vikiendelea kupamba moto.

Huku hayo yakijiri, ulimwengu unasubiri kusikia iwapo Rais wa Amerika Donald Trump ataamuru wanajeshi wa nchi hiyo kuungana na Israel katika kutekeleza mashambulio ya kuharibu vituo vya nuklia vya Iran.

Lakini Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu ameapa kwamba Israel itandelea kushambulia Iran hadi ifaulu kuharibu kabisa mitambo yake yote ya kutengeneza zana za kinuklia.

“Madikteta wa Iran watabeba gharama yote,” akasema.

Waziri wake wa Ulinzi, Israel Katz alisema wanajeshi wa nchi hiyo wameagizwa kuendeleza mashambulio ya angani katika vituo muhimu jijini Tehran ili kutokomeza kabisa tishio kwa Israel na kuvuruga “utawala wa Ayatollah.”

Netanyahu amesema mashambulio yanayotekelezwa na wanajeshi wa Israel huenda yakapelekea kuondolewa mamlakani kwa viongoni wa Iran.

Mashambulio ya wiki moja yaliyotekelezwa na Israel dhidi ya hasimu wake mkuu yameangamiza makamanda wa safu ya juu katika jeshi la Iran.