Makala

Ajuza, 80, ajiunga na chuo cha kushona; kwa weledi wake, wanamwita ‘Under 18’

Na SAMMY KIMATU June 20th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

AJUZA wa miaka 80 katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Kayaba, South B, Nairobi amewashangaza wengi baada ya kukiuka vikwazo vingi na kujiunga na kina mama wachanga kujifunza ushonaji.

Kutana na Grace Wamucii Rua mwenye umri wa miaka 80 aliyezaliwa Limuru mwishoni mwa Vita vya Pili vya Dunia mwaka wa 1945.

Kulingana na Grace, wazazi wake walikufa akiwa na umri wa miaka miwili.

Anasema kutokana na kuwa yatima, alichukuliwa na nyanyake yake kabla ya wajomba zake kumchukua na kumlea kama mtoto wao baada ya nyanyake kufariki.

Alikuja Nairobi Machi 1997.

Anasema hakujaliwa kupata mtoto hadi 1998 alipopanga (adoption) mvulana na msichana ambao alipewa na rafiki yake baadaye.

Amekuwa akiishi na watoto hao wawili Nairobi na amekuwa nao kama mama yao.

Leo, binti yake ameolewa na kubarikiwa mtoto ambaye Grace anasema ni ‘mtoto wake’.

Grace asema alikuwa Mkatoliki mwaminifu kabla kujiunga na Kanisa la All Nations PEFA South B.

Alisimulia jinsi alivyowasihi viongozi wa All Nations kupata nafasi shuleni au taasisi ya kujifunza ujuzi lakini kutokana na umri, hakuwa na bahati.

“Wasimamizi na walimu katika mradi wa Kushona Nguo walihisi nilikuwa mzee sana na kuongeza kwamba nitawapa walimu wakati mgumuna hivyo waliniambia sitoshi mboga na kunifukuza,” alisimulia.

Grace Wamucii Rua (kushoto) akifunzwa hatua za ushonaji nguo na mkufunzi Nancy Wafula katika Mradi wa Mafunzo wa PEFA South B Dorcas Tailoring & Dressmaking. Picha| SAMMY KIMATU

Hata hivyo, baada ya Askofu Munai kupata habari hizo, alimruhusu aingizwe darasani kwa sharti kwamba ataweza kusoma na kuandika.

Mwaka huu Grace alibainisha kuwa alikubaliwa katika kozi ya ushonaji ambayo imeratibiwa kwa mafunzo ya mwaka mmoja.

Alipoulizwa kwa nini alitaka kujifunza ushonaji wa mavazi, alisema alitaka kutumia ujuzi huo kama chombo cha kujikimu kimaisha.

Aliongeza kuwa tofauti na wanawake wengine ambao hufanya kazi katika makampuni kwenye Eneo la Viwanda na wengine ambao hufanya kazi za sulubu kama vile kupiga deki, kufua nguo na kuosha vyombo mitaani, yeye huchukizwa na kazi sampuli hiyo akisema hawezi kuwekwa katika makundi hayo.

“Nilichukia kufua nguo kwa malipo. Nilikuwa na ndoto ya kupata kazi nikitumia ujuzi wangu kama Mungu akinijali siku moja. Katika umri wangu siwezi kufua nguo za mtu. Ninataka kujitegemea,” akajibu kwa tabasamu.

Akiwa South B, alifanya kazi kama katika South B’s River Bank Estate ambapo alisimamia nyumba za makazi ambapo alihudumu miaka 16 huku mmiliki wa nyumba hizo akiwa ng’ambo.

“Nilikuwa nikisimamia nyumba za kupangisha katika mtaawa River Bank estate kwa miaka 16 lakini niliamua kupata ujuzi ambao unaweza kufanya maisha yangu ya baadaye kubadilika badala ya kuwa nikitengemea mtu kupita kiasi. Ninaamini katika kula jasho langu, ni tamu kuliko asali,” asema.

Leo anaishi mtaa wa mabanda wa Mukuru-Kayaba ulioko wadi ya Landi Mawe katika Kaunti Ndogo ya Starehe.

Mkufunzi Nancy Wafula wakati wa mahojiano katika Mradi wa Mafunzo wa PEFA South B Dorcas Tailoring & Dressmaking mnamo Juni 13, 2025. PICHA|SAMMY KIMATU

Ingawa aliripoti kwa mafunzo akiwa amechelewa kwa wiki mbili baada ya wanafunzi wengine kujiunga darasani, mkufunzi wake Bi Nancy Wafula alisema kuwa Bi Grace ni mchapakazi, mwanafunzi mtiifu na anayefanya kazi mithili ya mchwa, hata amemshangaza anapotekeleza kazi niliyomfunza.

“Mwanzoni, nilisitasita nikijiuliza maswali mengi, kama vile kuhusu umri wake ambao umepiku umri wa wazazi wangu kwa mbali nisijue kwamba hatupaswi kuhukumu kutokana na kipimo kutumia macho yetu. Bi Grace ni sogora zaidi kuliko baadhi ya wanafunzi wangu,” Bi Wafula alisimulia.

Akiwa darasani, Grace huketi kiti cha mbele ambapo hupenda kujifunza akiwa karibu na ubao.

Kulingana na Bi Wafula, Grace amepiga hatua kadhaa katika utengenezaji wa mavazi ambapo anajishughulisha na Mavazi ya Kike.

Mwanafunzi mwenzake, Binti Sarah Onyango, mwenye umri wa miaka 30, alimsifu Grace.

“Anasaidia katika kupanga nguo, hutupikia chai na ni mcheshi na hutupa ushauri sana. Jina la utani tunalomwita ni Under 18 na yeye ni bora,” Bi Sarah alijibu.

[email protected]