Mavazi manjano aliyovalia Wamuchomba yazua mchecheto bungeni
MBUNGE wa Githunguri Gathoni Wamuchomba aliibua mjadala bungeni Alhamisi, Juni 19, 2025, majira ya alasiri alipoibungia ukumbini akiwa amevalia mavazi, mkufu na viatu manjano, rangi ya chama tawala United Democratic Alliance (UDA).
Hata hivyo, sehemu ya shingo ya vazi lake ilikuwa nyeusi sawa na kitambaa alichokivalia kichwani.
Kinaya ni kwamba Bi Wamuchomba ni miongoni mwa wabunge waasi wa chama hicho kinachoongozwa na Rais William Ruto.
Mavazi ya manjano aliyovalia Bi Wamuchomba yalivutia hisia za kiranja wa wachache na mbunge wa Suba Kaskazini Millie Odhiambo aliyehoji iwapo vazi la mwenzake lilikuwa sawa kwa mujibu wa kanuni za mavazi yanayokubalika bungeni.
“Mheshimiwa Spika, naomba ufafanuzi ikiwa Mheshimiwa Wamuchomba amevalia sawasawa, kwani vazi lake ni la rangi ya chama cha kisiasa.
“Nguo yake ni manjano, viatu vyake ni manjano— kila kitu mwilini mwake ni manjano. Je, ni sawa kuvalia mavazi yenye rangi ya chama cha kisiasa bungen. Amevalia mavazi yenye rangi za UDA na hiyo ni kinyume cha Sheria za Bunge,” Bi Odhiambo akasema.
Kwa upande wake, Mbunge wa Dagoretti Kusini John Kiarie alishangaa ni vipi ni mbinu gani aliyotumia Bi Odhiambo kubaini kuwa “kila kitu mwili mwa Bi Wamuchomba ni manjano”.
“Mheshimiwa Spika inawezekanaje kwamba kile kitu mwilini mwa Mheshimiwa Wamuchomba ni manjano?. Sidhani kama madai hayo ni kweli,” akasema Mbunge huyo maarufu kama KJ.
Akijibu, Spika Moses Wetang’ula alisema malalamishi ya Bi Odhiambo, hayana msingi wowote, akisema maamuzi yake ya awali kuhusu kanuni kuhusu mavazi hitajika bungeni hayakupiga marufuku aina fulani za rangi.
“Katika taarifa yangu bungeni kuhusu jinsi wabunge wanahitajika kuvalia wakiwa bungeni, sikupiga marufuku mavazi ya rangi fulani. Kile hatutaki ndani ya ukumbi wa bunge ni alama au nembo za vyama vya kisiasa,” Bw Wetang’ula akasema.
“Spika hafai kuona rangi ya mavazi ya wabunge. Kwa hivyo, Mheshimiwa Wamuchomba amevalia sawasawa,” akaongeza.
Naye Bi Wamuchomba alinyanyuka na kumshtumu Bi Odhiambo kwa kuhoji mavazi kwa sababu alilenga kutathmini kwa undani Mswada wa Fedha wa 2025.
“Inasikitisha kuwa Millie anaweza kumwona Wamuchomba pekee akiwa amevalia rangi za UDA ihali hata nembo kwenye viti vyetu ni manjano,” Wamuchomba akasema.
“Lakini ni kwa sababu anajua kwamba niko hapa kuchambu Mswada wa Fedha ili kulinda masilahi ya Wakenya anaodai kuwatetea,” akaongeza.
Lakini Spika Wetang’ula alisema madai ya Mbunge huyo wa Githunguri hayana mashiko kwa sababu wabunge walikwisha kukamilisha kushughulikia Mswada wa Fedha na wakaupitishwa kwa baada ya kuidhinisha marekebisho yaliyopendekezwa na Kamati ya Bunge kuhusu Fedha.
“Ikiwa ulikuja kujadili Mswada wa Fedha wa 2025, basi ujue kwamba shughuli hiyo ilikamilishwa jana (Jumatano) na mswada huo sasa unabiri kuwasilishwa kwa Rais,” Bw Wetang’ula akamjibu.