Mtihani mgumu kwa UDA Mlimani
TANGAZO la mwenyekiti wa Devolution Empowerment Party (DEP) Lenny Kivuti kwamba chama hicho kitaunga mkono chama cha Democratic Party (DP) katika uchaguzi mdogo wa kuwania kiti cha ubunge cha Mbeere Kaskazini limefasiriwa kama pigo juhudi za UDA kutwaa kiti hicho.
Mnamo Mei 11, mwaka huu, katika mojawapo ya ziara zake nyingi katika Kaunti ya Embu, Naibu wa Rais Prof Kithure Kindiki aliapa kuhakikisha kuwa chama hicho tawala kinatwaa kiti hicho.
“Nitapiga kambi katika eneo la Mbeere Kaskazini hadi UDA ishinde. Serikali imerejesha kiti cha uwaziri katika eneo hili. Watu wa Mbeere wanafaa kushukuru kwa kumpigia kura mgombeaji anayeungwa mkono na serikali. Msiniangushe,” akasema katika uwanja wa Shule ya Upili ya Wasichana ya Siakago alipokutana na kundi la Wazee wa Jamii ya Mbeere.
Kiti cha ubunge cha Mbeere Kaskazini kilibaki wazi Aprili mwaka huu, Rais William Ruto alipomteua Geoffrey Ruku kuwa Waziri wa Utumishi wa Umma baada ya kumtimua Justin Muturi.
Endapo mahakama kesho, itatoa nafasi ya kuapishwa kwa mwenyekiti na makamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), wataanza maandalizi ya uchaguzi huo mdogo pamoja na chaguzi nyingine kadhaa.
Akiongea wiki jana katika kongamano la wajumbe wa DEP, Bw Kivuti ambaye ni seneta wa zamani wa Embu, pia alitangaza kuwa chama hicho kimejiunga rasmi na mrengo wa kisiasa unaoongozwa na aliyekuwa naibu wa rais Rigathi Gachagua na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka.
“Tumeamua kwamba baada ya rafiki yangu Muturi kupoteza nafasi ya uwaziri, tunapaswa kuunga mkono chama chake ili kishinde katika uchaguzi mdogo ikizingatiwa kuwa kiti hicho kilikuwa chake, kikishikiliwa na Geoffrey Ruku,” akasema Bw Kivuti.
Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa sasa wanabashiri kuwa uchaguzi mdogo wa Mbeere Kaskazini utageuzwa kuwa kura ya maamuzi dhdi ya chama tawala cha UDA na serikali ya Rais Ruto kwa jumla.
“Tangazo la Bw Kivuti linaashiria kuwa mrengo wa upinzani utaunga mkono mgombeaji wa kiti hicho kwa tiketi ya DP. Kwa hivyo, mgombeaji wa UDA atakuwa na nafasi finyu zaidi kutwaa ushindi ikizingatiwa kuwa umaarufu wake umedhoofika kufuatia kutimuliwa wa Muturi,” anasema Gitile Naituli.
Mapema mwaka huu, chama cha DEP kilichoanzishwa na aliyekuwa Gavana wa Meru Kiraitu Murungi kilikatiza uhusiano na muungano wa Kenya Kwanza kikidai masilahi yake hayakuwa yakizingatiwa.Hata hivyo, Bw Murungi, ambaye pia ni waziri wa zamani wa Haki na Masuala ya Kikatiba, sasa anahudumu serikalini kama Mwenyekiti wa Shirika la Kitaifa la Mafuta (NOC).
Baada ya chama hicho kutoa tangazo hilo, Rais Ruto alimwalika Bw Murungi katika Ikulu ya Nairobi kwa mashauriano.
Duru zinasema kuwa Rais alikubaliana na mwanasiasa huyo kwamba angewatunukia wanachama wa DEP nyadhifa mbalimbali serikalini “ili washirikishwe katika mpango wa utekelezaji wa ajenda za maendeleo za Kenya Kwanza.”
Hii ndiyo maana baada ya kutimuliwa kwa Bw Muturi Aprili mwaka huu, kulingana na Bw Kivuti, Dkt Ruto alimjulisha kuwa angetaka kumteua kujaza nafasi ya Waziri wa Utumishi wa Umma.
“Lakini nilikataa kwa sababu Muturi ni rafiki yangu na kuchukua nafasi yake ingekuwa sawa na kumsaliti,” Bw Kivuti akafichua wiki jana mbele ya wajumbe wa DEP.