Hizi debi tano zitakuwa moto EPL msimu ujao
JUMLA ya debi 50 zitasakatwa katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mnamo 2025-26 baada ya ratiba ya kampeni za kipute hicho muhula ujao kutolewa Jumatano iliyopita.
Debi ni mechi kati ya timu mbili zinazokaribiana kijiografia, ambazo mara nyingi huwa katika jiji, himaya au eneo moja, na ni wapinzani wakali kihistoria.
Ingawa hivyo, michuano kati ya Crystal Palace iliyo na makao yake jijini London na Brighton inayotokea huko Sussex, bado zinaitwa debi katika EPL licha ya umbali wa klabu hizo kijiografia.
Hii ni kwa sababu timu hizo zilikuwa na mazoea ya kukutana mara kwa mara katika miaka ya 1970s, ikiwa ni pamoja na mara tano katika msimu wa 1976-77.
Pia zimetenganishwa na Barabara ya M23, barabara moja ikiunganisha eneo la Sussex na London Kusini.
Mbali na mechi 42 zitakazotandazwa na vikosi saba (Chelsea, Palace, West Ham United, Fulham, Brentford, Tottenham Hotspur na Arsenal) katika Debi za London kati ya Agosti 17, 2025 na Mei 24, 2026; kuna debi nne nyingine maarufu katika EPL.
Manchester City watakuwa wenyeji wa Manchester United ugani Etihad mnamo Septemba 13 kabla ya kurudiana uwanjani Old Trafford kwenye Debi yao ya Manchester mnamo Januari 17, 2026.
Liverpool, ambao ni mabingwa watetezi wa EPL, watafungua Debi yao ya Merseyside dhidi ya Everton uwanjani Anfield mnamo Septemba 20 kabla ya kuelekea ugenini mnamo Aprili 18, 2026 kuumiza nyasi za Hill Dickinson Stadium ambao ni uwanja mpya wa Everton.
Kwenye Debi za Tyne-Wear, Sunderland wataalika Newcastle United uwanjani Stadium of Light mnamo Disemba 13 kabla ya limbukeni hao – waliorejea EPL mwishoni mwa muhula uliokamilika majuzi – kushuka ugani St James’ Park kwa gozi la marudiano mnamo Machi 21, 2026.
Brighton watakuwa ugenini katika uwanja wa Selhurst Park dhidi ya Palace kwenye mkondo wa kwanza wa Debi ya M23 mnamo Novemba 8 kabla ya vikosi hivyo kurudiana Februari 7, 2026 ugani American Express.
Chelsea ndio watafungua Debi za London kwa pambano litakalowakutanisha na Palace ugani Stamford Bridge mnamo Agosti 17.
Arsenal watafunga kampeni za EPL msimu ujao kwa Debi ya London itakayowakutanisha na Palace uwanjani Selhurst Park mnamo Mei 24, 2026.
Kisha watasubiri hadi Oktoba 4 kutandaza debi yao ya kwanza jijini London – dhidi ya West Ham – ugani Emirates.
Baada ya hapo, watakuwa wageni wa Fulham uwanjani Craven Cottage mnamo Oktoba 18 kabla kualika Palace kisha kukabiliana na mtihani mgumu wa Spurs (nyumbani), Chelsea (ugenini) na Brentford (nyumbani) kwa usanjari.
Spurs wataanza debi zao za London dhidi ya West Ham mnamo Septemba 13 uwanjani London Stadium, siku ambapo Chelsea watamenyana na Brentford ugani Gtech Community.
Kilele cha uzito wa kibarua cha Spurs katika debi hizo kitashuhudiwa Novemba ambapo watachuana na Chelsea (nyumbani), Arsenal (ugenini) na Fulham (nyumbani) mtawalia.
Debi yao ya mwisho itakuwa dhidi ya Chelsea ugani Stamford Bridge mnamo Mei 17, 2026.