Michezo

Kenya kuvaana na vigogo DRC mechi ya ufunguzi CHAN

Na CECIL ODONGO June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KENYA  itafungua mechi za Kundi “A” za Kombe la Afrika kwa wachezaji wanaoshiriki ligi za nyumbani (CHAN 2024) dhidi ya mabingwa mara mbili Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Mechi hiyo itagaragazwa katika uwanja wa Kasarani ambao una uwezo wa kuwasitiri mashabiki 55,000 kuanzia saa tisa mchana.

Kenya itakuwa mwenyeji wa kipute hicho pamoja na majirani Uganda na Tanzania. Timu nyingine ambazo zipo kwenye Kundi A ni Morocco, Angola na Zambia.

Kwenye kundi “B” Tanzania itavaana na Burkina Faso mnamo Agosti 2 kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa ambao una uwezo wa kuwasitiri mashabiki 60,000 na upo Dar es Salaam.  Timu nyingine za kundi hilo ni Madagascar, Mauritania na Jamuhuri ya Afrika ya Kati (CAR)

Uganda ambao wapo Kundi “C” wataanza mechi zao kwa kusakata dhidi ya Algeria Agosti 4 kwenye uwanja wa Nelson Mandela, Kampala wenye uwezo wa kuwasitiri mashabiki 45,202. Timu nyingine ambazo zipo kwenye Kundi  “C” ni Niger, Guinea na Afrika Kusini.

Mabingwa watetezi Senegal nao wataanza kutetea taji lao kwa kucheza dhidi ya Nigeria uwanja wa Amaan Zanzibar kwenye uwezo wa kuwapa hifadhi mashabiki 15,000. Mechi hiyo itasakatwa mnamo Agosti 5.

Uga wa Kasarani umeteuliwa kuandaa mechi ya fainali mnamo Agosti 30 nayo uwanja wa Nelson Mandela utakuwa mwenyeji wa mechi ya kusaka nafasi ya tatu.

Benjamin Mkapa, Tanzania ndio uwanja ambao utaandaa mechi ya kwanza na sherehe ya ufunguzi. Ni timu mbili pekee katika kila kundi zitafuzu robo fainali ambayo itasakatwa Agosti 22 na Agosti 23. Mechi za nusu fainali zitasakatwa mnamo Agosti 26.

Baada ya kucheza na DRC ambao walishinda Chan 2009 na 2016, Kenya ambayo inafundishwa na jagina wa soka wa Afrika Kusini Benni McCarthy itapumzika kwa siku tatu kabla ya kuvaana na Angola ugani humo Agosti 7

Mechi ya tatu ugani Kasarani itakuwa Agosti 10 uwanja wa Kasarani, Kenya ikichuana na Morocco ambao walishinda taji hilo mnamo 2018 na 2020.

Harambee Stars itahitimisha mechi zake za makundi dhidi ya Zambia uga huo huo wa Kasarani mnamo Agosti 17.

Uwanja wa Kitaifa wa Nyayo utakuwa mwenyeji wa mechi nyingine tano za Kundi “A” kisha mechi moja ya Kundi “C” kati ya Algeria na Niger mnamo Agosti 18.

Mechi za Kundi “A” ambazo zitaandaliwa Nyayo ni

Morocco vs Angola (Agosti 3), DRC vs Zambia (Agosti 7), Zambia vs Angola (Agosti 10), Morocco vs Zambia (Agosti 14) kisha DRC vs Morocco (Agosti 17).