Masuala tata katika mazungumzo kati ya ODM na UDA
SWALI la mgombea mwenza wa Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027, vyama tanzu kutengewa maeneo na utekelezaji wa ajenda ya vipengele 10 ni masuala yanayoibuka kuwa tata zaidi na yanayoweza kuvuruga mazungumzo ya muungano kati ya chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) na Orange Democratic Movement (ODM).
Ndani ya ODM, mvutano mkali wa kuwania uwakilishi wa kimaeneo pia umeibuka. Wabunge kutoka Pwani wamesema hadharani Waziri wa Madini Hassan Joho ajumuishwe katika mazungumzo hayo.
Aidha, Taifa Jumapili imebaini kuwa Gavana wa Kisii Simba Arati na Waziri wa Ushirika Wycliffe Oparanya pia wametoa madai sawa kwa niaba ya maeneo yao.
UDA na ODM, kupitia kamati mbalimbali, vimeidhinisha Rais William Ruto na Oburu Oginga kuunda kikosi cha kufanikisha mazungumzo.
Hata hivyo, maslahi yanayokinzana yanayoibuka yanaonekana kupunguza kasi ya mchakato huu, huku pande zote zikifanya mashauriano mapana.
Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Junet Mohammed aliambia Taifa Jumapili kuwa ODM bado haijateua timu ya mazungumzo.
Hata hivyo, hakutoa sababu ya kuchelewa kufanya hivyo.
Makamu mwenyekiti wa ODM na Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo, Jumamosi iliyopita alimuomba Dkt Oginga asiwe sehemu ya timu ya mazungumzo bali awaruhusu maafisa wa ngazi za chini waongoze mchakato huo.
“Sote tunataka mazungumzo yenye mpangilio. Lakini tunapoingia kwenye mazungumzo haya, unapaswa kukaa kando na kuwaacha askari wako wachukue usukani,” alisema Dkt Amollo.
ODM kupitia Kamati Kuu Simamizi (CMC) iliidhinisha mazungumzo ya muungano na UDA mnamo Januari 12.
Mnamo Ijumaa alipozuru Kisumu, ngome ya ODM, Rais Ruto aliomba eneo hilo limruhusu kufanya mazungumzo, akisema ana maslahi ya eneo hilo moyoni.
“Leo naomba ruhusa yenu, watu wa Kisumu, kuruhusu UDA na ODM kufanya kazi pamoja na kuunda serikali ijayo.
Mniruhusu niketi na Dkt Oburu Oginga tupange serikali mpya itakayomaliza ukabila na uongozi mbaya,” alisema Dkt Ruto katika akiwa Kondele, Kisumu.
Ugavi wa madaraka, ikiwemo nyadhifa muhimu serikalini, pia unaibuka kuwa suala nyeti, huku baadhi ya watu ndani ya UDA wakipambana kulinda nafasi zao.
ODM kupitia Dkt Oginga imedai nafasi ya mgombea mwenza wa urais kama sharti lisiloweza kujadiliwa ili kumuunga mkono Rais Ruto kuchaguliwa tena. Msimamo huu unaonekana kupingwa na washirika wa Naibu Rais Kithure Kindiki.
Profesa Kindiki anasisitiza adumishe wadhifa wake serikalini kama njia ya kuvutia eneo lenye idadi kubwa ya wapiga kura la Mlima Kenya kumuunga mkono Dkt Ruto katika uchaguzi ujao.
Mlima Kenya pamoja na Bonde la Ufa vilimpa Dkt Ruto ushindi mwaka 2022.
Hata hivyo, eneo hilo linaonekana kuanza kujitenga na UDA kufuatia kuondolewa madarakani kwa Rigathi Gachagua kama Naibu Rais.
Mwenyekiti wa Kitaifa wa UDA na Gavana wa Embu Cecily Mbarire aliweka mwelekeo katika kikao cha Baraza Kuu Simamizi la Kitaifa la UDA kwa kutetea wazi Kindiki kama mgombea mwenza wa Dkt Ruto mwaka 2027.
Bi Mbarire alisema Profesa Kindiki amepatia serikali mwamko mpya ambao Rais alikosa alipokuwa na Bw Gachagua kama naibu wake.
“Wewe (Kindiki) unaungwa mkono na UDA nzima na vyama washirika. Naibu Rais ametupa mwamko mpya kwa kauli mbiu ya ‘faya si faya’. Pia amekuwa akizunguka nchi nzima akielezea miradi ya serikali bila hofu,” aliongeza.
Seneta wa Tana River Danson Mungatana naye alieleza hofu kuwa “watoto wa nyumba” huenda wakasahaulika katika mazungumzo na ODM.
“Tunapoingia katika mazungumzo yenye mpangilio, sisi watoto wa nyumba tuna wasiwasi mkubwa kwa sababu mara nyingi walio ndani husahaulika wanapoingia wa kutoka nje,” alisema Bw Mungatana.
Hata hivyo, Rais aliepuka kutoa ahadi yoyote kuhusu mgombea mwenza.
Badala yake, alisema UDA itabaki na kiti cha juu—urais—na akaahidi mazungumzo ya kufaidi pande zote.
“Namwambia Mungatana kwamba katika mazungumzo yaliyofanyika hadi sasa, urais bado uko UDA. Sidhani kuna nafasi kubwa zaidi ya kufikiria kuliko urais,” alisema.
Profesa David Monda, mhadhiri wa chuo kikuu nchini Amerika na mchambuzi wa siasa, anasema mazungumzo yataathiriwa kwa kiasi kikubwa na madai ya ODM, pamoja na utekelezaji wa ajenda ya vipengele 10.
Pia, hofu imeibuka ndani ya ODM kwamba vyama vingine, ikiwemo vinavyoshirikiana katika serikali jumuishi, vinatumia ukaribu huo na kutokuwepo kwa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kupenya ngome zake za jadi.
UDA, DAP-K cha aliyekuwa Waziri Eugene Wamalwa, UPA kinachohusishwa na aliyekuwa Waziri Fred Matiang’i, na Movement for Democracy and Growth cha Mbunge wa Ugenya David Ochieng’, ni miongoni mwa vyama vinavyolenga Nyanza, Gusii, Magharibi na Pwani.
Kwa msingi wa hofu hiyo, ODM kupitia Mwenyekiti wake wa Kitaifa Gladys Wanga na vigogo wengine wanataka kutengwa kwa maeneo ndani ya mpangilio wa serikali jumuishi ili kulinda ngome zao. Wadau wa ndani wanaamini ni kwa kubaki na ngome hizo ndipo ODM itakuwa na nafasi halisi katika serikali ijayo.
Hata hivyo, madai hayo yamewashtua baadhi ya wanachama wa UDA katika maeneo ya ODM, na pia baadhi ya wanachama wa ODM wanaotaka chaguo mbadala iwapo watanyimwa haki katika kura za mchujo.
Mwenyekiti wa UDA Kaunti ya Homa Bay Kennedy Obuya alihoji kwa nini ODM inataka kukandamiza demokrasia ya vyama vingi ilhali inadai kuipigania. Alisema madai hayo yanaashiria hofu ya ushindani wa kisiasa.