Jamvi La Siasa

KINAYA: Ama tumwambie Rais Trump anunue Kenya tugawane pesa?

Na DOUGLAS MUTUA February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

AKILI mtu wangu! Lazima uzifanyishe kazi ili maisha yakunyookee, uache kuishi maisha uchwara yasiyotamanisha hata kidogo.

Ikiwa umechoshwa na Kenya, na unatamani iuzwe kisha tugawane pesa, ila umekosa mteja, nitafute tuongee.

Nadhani Rais Donald J. Trump wa Amerika anaweza kuinunua Kenya, na ziada amlipe kila Mkenya milioni kadha, tena aturuhusu kuendelea kuishi Kenya kama raia wa Amerika.

Hilo likifanyika, hutahitaji kuomba kibali cha kuzuru Amerika kwa sababu Amerika yenyewe itakuwa imejileta kwako, ikakuletea na mafedha tele.

Ndoto yako ya kuwa milionea inaweza kutimia haraka kuliko unavyofikiria.

SOMA PIA: KINAYA: Tutaishi kushiriki vitimbi na sarakasi au tutajenga nchi?

Wazo hili limenijia baada ya kupiga soga na Mwamerika mjanja anayetaka kuhamia Kisiwa cha Greenland, kilicho milki ya taifa la Denmark, na ambacho Trump anamezea mate.

Rais huyo nusu-kichaa hivi majuzi ameiambia Denmark kwamba afua ni mbili: ama akitwae kisiwa chenyewe kijeshi, au akinunue Dola 700 bilioni (Sh90 trilioni) na kumpa kila mkazi Dola Laki Moja (Sh13 milioni)!

Mwamerika rafiki yangu ananiambia ananuia kuhamia kisiwa hicho kikubwa zaidi duniani ili kikinunuliwa apate hela hizo kama mkazi, wala hatahitaji kurejea kwake kwa sababu tayari Greenland itakuwa sehemu ya Amerika mpango huo ukiiva.

Ukizingatia hali hiyo, hudhani mnunuzi wa Kenya amepatikana? Kazi iliyosalia ni wewe tu kumrai kwa ahadi kwamba nchi tunayomuuzia ina utajiri mwingi wa mafuta, dhahabu, almasi na madini mengineyo.

Pia unaweza kumtishia kwa kumwambia kuwa Uchina na Urusi zinatamani bidhaa hizo, hivyo aharakishe kufanya maamuzi yake ya kununua Kenya kabla washindani hao hawajatoa donge nono kumzidi na hivyo basi kumzuia kutawala Afrika Mashariki anavyotaka.

SOMA PIA: KINAYA: Kiburi cha Krismasi kimeisha huku vijijini, nina hakika uko tayari kurejea mjini!

Mpango huo ukiiva, utakuwa umeondolea Wakenya wengi umaskini, sarafu ya pesa zetu iwe dola badala ya shilingi, Afrika nzima mtu akitaka kwenda Amerika aendeshe gari au avuke mpaka kwa mguu na kuingia Jimbo la Kenya!

Wewe pia utakuwa huru kuishi sehemu yotote ya Amerika, si lazima ukwame ulipo sasa hivi. Labda miji mikubwa kama New York, Washington, D.C. na kadhalika inakutamani na kukuhitaji kuliko unavyoitamani na kuihitaji.

Akili mtu wangu!

Hata hivyo, kwanza tuulizane swali hili: Kwa nini Kenya iuzwe tugawane pesa? Kenya kuna mambo mengi ya kuudhi na kuzuga watu akili.

Mathalan, kuna hili ambalo limewaudhi watu wengi la mtu aliyetangaza kadamnasi ya watu kwamba kwa hiari yake mwenyewe havai chupi, kisha kampuni fulani za kuuza chupi zikampa mkataba wa kutangaza chupi ili zinunuliwe.

Watu ambao siku zote wamekuwa wakivaa chupi wanauliza kwa nini atafutwe asiyevaa ili anadi bidhaa hiyo ilhali wenyewe wamevaa siku zote bila shuruti?

SOMA PIA: KINAYA: Wanaume wazuiwe kuchagua ‘mama kaunti’ almaarufu ‘Woman Rep’

Kwa nini wasipewe fursa hiyo? Mbona wananyimwa fursa, halafu inapewa asiyeitaka?

Hata vijana wa Mungich (Mungiki) ambao kamwe hawavai chupi wanauliza, ikiwa wasiovaa wanazawadiwa kwa kazi za kufanya matangazo ya biashara, mbona wao wasipewe fursa hiyo ilhali tangu hapo polisi wakiwatambua na kuwakamata kwa kutovaa?

Ukitafakari kuhusu mjadala huu, halafu ukumbuke SHA haikuhudumii inavyostahili, hutapewa bila malipo nyumba za gharama ya chini zinazojengwa na serikali kwa hela zako, ongeza na Januari ambayo nusra ikuue kwa njaa, unatamani Trump anunue Kenya mara moja!

Usione ugumu wowote kutumia akili mtu wangu.

mutua_muema@yahoo.com

UNAWEZA KUPENDA: Usimtishie mbunge wako bila vitendo, jisajili kupiga kura