MAONI: Kuna hatari kuu Kenya kuiga Tanzania, Uganda uchaguzini
KUFUATIA misururu ya chaguzi kuu za mataifa mawili ya Afrika Mashariki – Tanzania, Uganda, kuna motifu ya aina fulani ambayo inadhihirika wazi.
Katika taaluma ya fashihi, dhana ‘motifu’ hutumiwa kuelezea elementi fulani za kimuundo au kimaudhui inayotawala kazi ya kifasihi. Katika uchaguzi mkuu wa Tanzania wa Oktoba 29,2025, ambapo Rais Samia Suluhu ‘aliibuka mshindi’, ghasia, fujo na sokomoko zilikumba taifa hilo, ambalo kwa miaka na dahari lilionekana kuwa kielelezo cha demokrasia.
Kwenye uchaguzi mkuu wa Uganda uliofanyika Januari 15, 2026, Yoweri Kaguta Museveni – ambaye ameitawala nchi hiyo tangu 1985 alimbwaga mpinzani wake, Bw Bobi Wine.
Bw Museveni alizoa asilimia 72 ya kura, dhidi ya Bw Wine, aliyepata asilimia 25 kwenye uchaguzi huo, ambao pia ulikumbwa na utata ulioandamana na rabsha.
Chambacho wahenga, mwenzako akinyolewa, tia (kichwa) chako maji. Ghasia na wizi wa kura ni mambo yanayofanana katika chaguzi za Tanzania na Uganda.
Kenya, ambayo inajiandaa kwa uchaguzi mkuu utakaofanyika Agosti 10, 2027 inapaswa kujifunza nini kutokana na chaguzi za Tanzania na Uganda?
Mazingira ya kisiasa Kenya ni tofauti na ya nchi hizo mbili. Hivi sasa, dira ya siasa za Kenya inaendelea kulisukuma taifa hili kuelekea kwenye mkondo wa kani ya ‘mageuzi’ yaliyosababishwa Generation Zoom (Gen Z) mnamo Juni 2024.
Taathira ya mageuzi hayo nchini Kenya inaonekana wazi kuwili. Kwanza, siasa za ukabila ambazo zimekita mizizi katika nchi nyingi Afrika, tangu uhuru hasa nchini Kenya zimeonekana kuyumbayumba.
Pili, vuguvugu la Gen Z lilikwisha kusogeza ‘kitovu sumbufu’ cha siasa zinazonufaika na kani ya ukabila, na kuchochea mdahalo wa uwazi na uwajibikaji serikalini na uongozini.
Yamkini kuna dalili za wazi nchini Kenya kwamba, makabila yote huenda yakaungana kupinga dhuluma, ubarakala na ukiritimba wa wanasiasa – ambao hutegemea kutumia karata ya ukabila kudumisha maslahi yao.
Kwa mfano, katika tamthilia ya Kinjeketile (OUP, 1969) iliyotungwa na Ebrahim Nurdin Hussein wa Tanzania, manokoa wanaolazimishwa kufanya kazi za unokoa katika mashamba ya Mjerumani wanagutushwa na Kinjeketile Ngwale kuhusu unyonge wao wanapokubali kugawanywa katika misingi ya kikabila.
Vita vya ukombozi wa Watanganyika kutoka kwa utawala dhalimu wa Wajerumani vilikumbwa na matatizo kadha wa kadha.
Katika muktadha wa uchaguzi mkuu wa Kenya mnamo 2027, kuna kila dalili kwamba ukabila utakuwa na kani dhaifu mno katika kinyang’anyiro hicho.
Bitugi Matundura ni mhadhiri Chuo Kikuu cha Chuka