Aliyejaribu kuua Trump afungwa jela maisha
Mwanamume aliyepanga kumfyatulia risasi Rais wa Amerika Donald Trump ataishi gerezani maisha baada ya kupatikana na hatia ya kujaribu kumuua kiongozi huyo katika uwanja wa gofu mwaka 2024.
Ryan Wesley Routh, mwenye umri wa miaka 59, alihukumiwa kifungo cha maisha jela pamoja na miezi 84 ya ziada katika gereza la shirikisho na Jaji Aileen M Cannon katika uamuzi uliotolewa Februari 4 2026.
Hukumu hiyo ilitolewa baada ya Routh kupatikana na hatia katika mashtaka yote matano yaliyomkabili, likiwemo la kujaribu kumuua Trump.
Tukio hilo lilitokea katika Klabu ya Gofu ya Trump International mnamo Septemba 2024, wakati maafisa wa Idara ya Usalama wa Rais walipomwona Routh akiwa amejificha kando ya ua wa uwanja huo.
Afisa wa ujasusi, Robert Fercano alimuona Routh akiwa ameelekeza bunduki iliyofanana na AK-47 kutoka mafichoni kando ya uwanja wa gofu.
Kwa kuogopa maisha yake na usalama wa Trump, afisa huyo alimfyatulia risasi Routh, hali iliyomlazimu mshtakiwa kutoroka eneo hilo mara moja.
Baadaye, maafisa wa usalama walipata bunduki aina ya Norinco SKS yenye darubini na iliyojaa risasi katika eneo alilokuwa. Bunduki hiyo ilikuwa na risasi 19 na risasi moja tayari kufyatuliwa wakati wowote.
Maafisa pia walipata kamera iliyokuwa imefungwa kwenye ua, ikielekezwa moja kwa moja Trump alikopangiwa kucheza gofu.
Shahidi mmoja aliripoti kumuona Routh akikimbia kuvuka barabara na kuingia kwenye gari aina ya Nissan Xterra jeusi baada ya tukio hilo. Kwa kutumia taarifa hiyo, maafisa walimkamata Routh alipokuwa akielekea kaskazini kwenye barabara kuu ya Interstate 95.
Upekuzi katika gari lake ulipata simu kadhaa za mkono ambazo ukaguzi wa kina uligundua kuwa Routh alikuwa akifuatilia mienendo ya Trump kwa karibu mwezi mmoja kabla ya jaribio la mauaji na maelezo yaliyoonyesha alipanga kuondoka Amerika.
Aidha, wachunguzi walipata barua iliyoandikwa kwa mkono na Routh na kuachwa katika nyumba ya shahidi mnamo Aprili 2024, ikieleza wazi kuwa kitendo hicho kilikuwa jaribio la mauaji.
Mwanasheria Mkuu wa Amerika, Pamela Bondi, alisema jaribio hilo la kumuua Rais Trump halikuwa tu shambulio dhidi ya rais bali pia dhidi ya mfumo mzima wa kidemokrasia wa Amerika.
Kesi hiyo ilisikilizwa kwa wiki mbili katika mji wa Fort Pierce, Florida, kabla ya jaji kumpata Routh na hatia katika mashtaka yote.