Gavana anavyoimarisha maisha ya vijana kupitia ufugaji wa nguruwe
KATIKA kijiji cha Gikuni, Wadi ya Nyathuna, Kabete, Kaunti ya Kiambu, sauti za nguruwe wakisaka chakula kwenye mazizi yao zimetwaa nafasi ya ukimya uliokuwa umetawala vijana wasio na ajira ya kudumu.
Ni ishara ya mageuzi ya kiuchumi yanayoendelezwa na Serikali ya Gatuzi la Kaunti ya Kiambu, chini ya Gavana Kimani Wamatangi kupitia mpango wa kupiga jeki sekta ya kilimo.
Kando na programu ya usambazaji pembejeo za kilimo kama vile fatalaiza na mbegu, Gavana Wamatangi pia anaendeleza mpango wa usambazaji vivinimbi – wana wa nguruwe, kwa vijana.

Kwa Peter Gitau, mwekahazina wa kikundi cha vijana eneo la Gikuni, mradi huo umewaletea mabadiliko makubwa.
Baada ya kikundi chao kupokea wana wa nguruwe kutoka kwa serikali ya kaunti, walikodisha sehemu na kuanza ufugaji. Kilichoanza kama msaada mdogo sasa kimestawi na kuwa biashara endelevu inayowapa vijana mapato, mwelekeo na matumaini mapya. “Sisi si wavivu tena. Hawa nguruwe wametufanya tuwe na bidii,” anasema Gitau.
Kikundi cha Kirangari Self Help Group, kinachojumuisha wanachama waliokuwa makanga wa matatu, ni miongoni mwa walionufaika na mpango wa Gavana wa Kiambu.

Leo hii, wamegeuza ufugaji wa nguruwe kuwa biashara inayowaunganisha na kuwainua kiuchumi.
Mwenyekiti wao, Joseph Kaniaru, anasema mradi huo umeimarisha utangamano wa kundi na kuwavunia heshima katika jamii.
Hadithi kama hiyo, inawiana na ya Gatukuyu, Wadi ya Mangu, ambako Augustine Gathii, mwenye umri wa miaka 28, alipokea mtoto wa nguruwe baada ya kuhudhuria mkutano wa Gavana Wamatangi. Ndani ya miezi minane, nguruwe huyo amejifungua mara mbili na Gathii sasa ana jumla ya nguruwe saba.

Amejifunza kutengeneza chakula cha mifugo, kudumisha usafi na anapanga kupanua biashara yake – awe na zizi kubwa kwa kuongeza idadi ya nguruwe.
“Baada ya kuhudhuria mkutano wa Gavana, nilirejea nyumbani si tu na nguruwe pekee, bali pia na matumaini mapya,” anasema.
Mita chache kutoka kwake, jirani yake Boniface Mburu, mwenye miaka 25, anakiri mpango huo kuokoa maisha yake baada ya kukosa ajira kwa muda mrefu.

Nguruwe aliopewa mwaka 2025, amejifungua watoto wanane, wawili kati yao tayari wameuzwa na mapato yake kutumika kuboresha mradi na kununua chakula zaidi.
Ni simulizi zinazohinikiza karibu kila sehemu ya Kiambu.
Katika wadi zote 60, mamia ya vijana wanakumbatia kilimo-biashara kupitia mpango wa serikali ya kaunti kuwapiga jeki.
Mbali na kusambaza nguruwe, serikali ya gatuzi la Kiambu inatoa mafunzo, huduma za mifugo na kuanzisha masoko.

Matokeo yake ni wazi: maduka ya chakula cha mifugo yanastawi, mafundi wanajenga mazizi, mabanda, na maafisa wa afya ya wanyama – mavetinari wanahitajika zaidi.
Gavana Kimani Wamatangi anasema mpango huo unalenga kuhusisha vijana na wanaume katika ufugaji wa nguruwe kama njia ya kuwafanikisha kiuchumi, ikizingatiwa kuwa nguruwe mmoja anaweza kuzaa hadi watoto 15 kwa kizazi kimoja.

Waziri wa Kilimo, Ufugaji na Samaki katika Kaunti, John Kuria, anaongeza kuwa mpango huo unapania kubadilisha maisha ya vijana ambao mara nyingi husahaulika.
“Tumeshuhudia hadithi tele za ufanisi miongoni mwa vijana, baada ya kuanzisha mradi huu.”
Anaamini, chini ya miezi kadhaa ijayo 2026 simulizi hizo zitasaidia kuboresha maisha ya vijana wa Kiambu, kaunti anayosema ni nadra ikigonga vichwa vya habari kwa mada za ukuaji.
