Makala

Pasta Natasha afichua alilipa mahari ya Sh17 milioni kupata mume

Na ELIZABETH NGIGI February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MHUBIRI maarufu Lucy Natasha, anayejulikana kwa jina la Oracle, amefichua wazi safari yake ya imani, ndoa ya tamaduni tofauti iliyomgharimu Sh17 milioni kama mahari, pamoja na uamuzi wa kuhamishia kanisa lake mtandaoni.
Pasta Natasha, mchungaji mkuu wa Empowerment Christian Church (ECC), anasema wito wake hauwalengi watu wote bali hasa vijana wa kizazi cha milenia na Gen Z.
Pasta Natasha anaeleza kuwa alikutana na mumewe, Carmel, akiwa kwenye safari ya kuhubiri kaskazini mwa India.
Mawasiliano yao yalianza kupitia ujumbe mfupi, kisha yakakua taratibu hadi kuwa uhusiano wa kimapenzi. Carmel, anayeishi Canada, alimvutia kwa unyenyekevu na uangalifu, tofauti na lugha za kiroho ambazo Natasha alikuwa amezoea kusikia.
Walifunga ndoa mwaka wa 2022, lakini kutokana na tofauti za kitamaduni kati ya Kenya na India, walilazimika kufuata taratibu za pande zote mbili. Natasha anakiri kuwa katika utamaduni wa India, mwanamke ndiye hulipa mahari, tofauti na Kenya ambako jukumu hilo ni la mwanaume.
Hatimaye, mwaka wa 2025, alisafiri hadi Kerala, India, ambako alilipa mahari kwa familia ya mumewe ya thamani ya takriban Sh17 milioni.
“Sikuwahi kufikiria kuwa siku moja ningelipa mahari kwa mwanaume, lakini ndivyo ilivyotokea. Mwaka wa 2025, nilifanya harusi ya kitamaduni nchini India. Nilisafiri pamoja na baadhi ya wanafamilia wangu na tukalipa mahari huko Kerala, kusini mwa India,” alisema.
Alisema katika utamaduni wa Wahindi, mahari hulipwa hasa kwa dhahabu, ingawa thamani yake inaweza kubadilishwa na kuwa pesa taslimu.
“Kwa upande wetu, tulitoa pesa, zawadi mbalimbali, mavazi na bidhaa nyingine kulingana na mila. Kiasi nilicholipa kilikuwa ni takriban Sh17 milioni,” alisema.
Akicheka, alisema tukio hilo lilimfundisha mengi kuhusu ndoa za tamaduni tofauti. Aliwashauri wanawake ambao bado hawajaolewa na wanafikiria kuolewa na wanaume kutoka India kuhakikisha wamejiandaa kifedha.
Anasema uzoefu huo ulimfundisha umuhimu wa maandalizi katika ndoa, hasa zile za tamaduni tofauti.
Licha ya changamoto za ndoa ambayo wachumba wanaishi maneo tofauti, Natasha anasema wana uhusiano wa karibu, husafiri pamoja mara kwa mara na hawaathiriwi na kelele za mitandao ya kijamii.
Pasta Natasha pia amezungumzia mtindo wake wa mavazi, akisema kuwa kuonekana nadhifu na kuvutia hakukinzani na kumtumikia Mungu.
Anasema anazungumza lugha ya vijana anaowaongoza, akiamini kuwa injili inaweza kubadilisha maisha ya mtu bila kumlazimisha kubadilika kwa nje kwanza.
Mhubiri huyo alipata umaarufu mwaka wa 2017 alipoanzisha ibada iliyovutia maelfu ya waumini kutoka madhehebu mbalimbali.
Mtindo wake wa kuhubiri, mavazi ya kisasa na lugha inayovutia vijana vilimtofautisha na wahubiri wengine.
Kanisa la ECC lilianzishwa rasmi Februari 2021 na lilikuwa likiendesha ibada katika paa la jengo moja katikati ya jiji la Nairobi.
Hata hivyo, kutokana na ongezeko kubwa la waumini na changamoto za kimuundo kama ukosefu wa nafasi ya maegesho, uongozi wa kanisa uliamua kusitisha ibada za ana kwa ana na kuhamishia shughuli nyingi mtandaoni.
Natasha anasisitiza kuwa kanisa si jengo bali ni watu, imani na uwepo wa Mungu, akiongeza kuwa huduma yake bado inaendelea kupitia mikutano, makongamano na mahubiri ya kimataifa.
Anakiri kuwa kuendesha injili ni gharama kubwa.
Kodi ya eneo la ibada ilikuwa Sh350,000 kwa mwezi, ambayo kwa miaka mitano ilifikia takriban Sh22 milioni.
Zaidi ya hayo, vifaa vya sauti viligharimu Sh10 milioni na vya vyombo vya habari Sh15 milioni, bila kusahau mishahara ya wafanyakazi 20 wa kudumu, huku zaidi ya watu 100 wakihudumu kwa kujitolea.
Mapato ya kanisa yalitokana na sadaka na michango ya waumini waliokuwa wamejumuika mtandaoni, hasa baada ya janga la Covid-19 kusitisha mikusanyiko ya ana kwa ana. Anasema waumini waliitikia wito wa kuchangia, hali iliyowezesha ukarabati na ujenzi wa patakatifu.