Siasa

Mwelekeo ni upi ODM? Kundi la Linda Mwananchi lakabili Linda Ground

Na BENSON MATHEKA February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MVUTANO ndani ya Chama cha ODM sasa umeingia katika awamu mpya baada ya kuzinduliwa kwa mpango wa Linda Mwananchi, unaotajwa waziwazi kama jibu la kisiasa kwa mikutano ya Linda Ground inayoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Hatua hii imeweka wazi mgawanyiko mkubwa ndani ya chama, huku kambi pinzani zikikabiliana kuhusu mwelekeo wa ODM, uwazi wa kifedha na uhusiano wake na serikali ya Kenya Kwanza kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Mpango wa Linda Mwananchi unaongozwa na Katibu Mkuu wa ODM na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, pamoja na wabunge na maseneta wanaopinga muungano wa ODM na United Democratic Alliance (UDA).
Ziara hiyo ya kisiasa inatarajiwa kuanza rasmi Busia mnamo Februari 8, na inalenga kuhamasisha wananchi mashinani kuhusu masuala ya gharama ya maisha, uwajibikaji wa serikali, haki za raia na nafasi ya ODM kama chama cha upinzani.
Ingawa wanaotarajiwa kuhudhuria mkutano wa leo wote si wanachama wa ODM, kuibuka kwa Linda Mwananchi kunajiri wakati ambapo mikutano ya Linda Ground, inayohusishwa na kambi inayoongozwa na Seneta wa Siaya Oburu Odinga, imekuwa ikiendelea kwa kasi.
Mikutano hiyo inalenga kukusanya maoni ya wanachama wa ODM kuhusu uamuzi wa Kamati Kuu ya Usimamizi wa chama kuingia katika makubaliano ya kisiasa na UDA kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Mkutano huo unafanyika wiki chache baada ya ule wa Linda Ground, kuonyesha tofauti zinazoendelea kupanuka katika chama hicho.
Hata hivyo, kile kilichoanza kama mjadala wa sera sasa kimegeuka kuwa mzozo wa wazi, hasa baada ya Sifuna kudai hadharani kuwa chama cha ODM hakijatumia hata shilingi moja kufadhili mikutano ya Linda Ground, licha ya gharama kubwa inayoonekana kutumika.
“Ninaweza kusema kwa mamlaka kamili kuwa fedha mnazoziona zikitumika katika mikutano hiyo hazitoki makao makuu ya ODM,” alisema Sifuna katika mahojiano ya televisheni.
“Mimi ni mtia saini wa akaunti za chama. Fedha ya mwisho tuliyotumia rasmi ilikuwa sherehe za miaka 20 ya ODM Mombasa, na ilikuwa kiasi kidogo sana ikilinganisha na kile kinachoendelea sasa.”
Kauli hizo ziliibua hasira kutoka kwa baadhi ya wanachama wa ODM waliomlaumu Sifuna kwa kusaliti chama na kuonekana kupinga uongozi.
Lakini mashambulizi hayo yamekabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa Mbunge wa Wanawake wa Kisumu, Ruth Odinga, dada wa marehemu Raila Odinga.
Kupitia mtandao wa Facebook, Ruth aliwataka wanachama wa ODM waache kushambulia Sifuna na badala yake wajibu maswali anayouliza.
“Ikiwa Katibu Mkuu wa chama anauliza pesa za helikopta, mahema makubwa, fulana na kofia za ODM kwenye mikutano ya Linda Ground zinatoka wapi, ni kosa gani hilo?” alihoji Ruth.
“Amekiri hadharani kuwa ODM haijatumia hata senti moja. Wenye majibu, kwa nini hamjitokezi?”
Ruth alihoji ikiwa ni magavana, wabunge au wafadhili wasiojulikana wanaofadhili mikutano hiyo, na kama kuna maslahi ya kisiasa au kiuchumi yanayofuatwa kwa siri. Alionya kuwa chama kinapozima mjadala wa ndani na kuwatisha wanaouliza maswali, kinajitenga na misingi ya demokrasia ambayo ODM ilijengwa.
Mbali na suala la fedha, Ruth pia aliibua swali la uaminifu wa makubaliano ya kisiasa na Rais Ruto, akisema ikiwa MoU ya sasa haijaheshimiwa na muda uko karibu kuisha, hakuna msingi wa kuamini ahadi nyingine za kisiasa.
“Ikiwa Rais hakuheshimu makubaliano aliyotia saini na Raila Odinga, ni nini kinachowafanya muamini ataheshimu makubaliano ya kabla ya uchaguzi?” aliuliza.
Kwa upande wa Linda Mwananchi, msimamo wao ni kwamba ODM haipaswi kuingia katika muungano wa kudumu na serikali, bali ibaki kuwa sauti ya wananchi wanaokabiliwa na gharama ya juu ya maisha, ushuru mzito na ukosefu wa ajira.
Miongoni mwa viongozi wanaotarajiwa kushiriki ziara hiyo ni Maseneta Richard Onyonka (Kisii), Godfrey Osotsi (Vihiga) na Erick Okong’o Mogeni (Nyamira), pamoja na wabunge kama Babu Owino, Caleb Amisi, Wanami Wamboka, Patrick Makau na Joshua Kimilu.
Kwa upande mwingine, viongozi wanaounga mkono Linda Ground wanasema mikutano hiyo inalenga umoja wa chama na utulivu wa kisiasa, wakisisitiza kuwa mazungumzo na serikali ni muhimu kwa maslahi ya taifa.
Hata hivyo, Naibu Kiongozi wa ODM Godfrey Osotsi amelalamika kuwa hakuhusishwa katika maandalizi ya baadhi ya mikutano hiyo licha ya wadhifa wake wa juu, ishara nyingine ya mgawanyiko uliopo.
Kulingana na wachambuzi wa siasa, kuibuka kwa Linda Mwananchi dhidi ya Linda Ground kunaashiria zaidi ya tofauti za kimtazamo na ni mapambano ya hatima ya chama, nafasi yake katika siasa za kitaifa, na uhusiano wake na wananchi kuelekea 2027.