Kimataifa

Mmiliki wa mochari ahukumiwa miaka 40 jela kwa kudhulumu maiti

Na MASHIRIKA February 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MMILIKI mwenza wa mochari katika jimbo la Colorado ambako karibu miili 200 iliyokuwa ikioza ilipatikana, amehukumiwa kifungo cha miaka 40 gerezani kwa kosa la kudhulumu maiti.
Kabla ya hukumu kutolewa, Jon Hallford aliomba msamaha mahakamani na kusikiliza familia za waathiriwa zikisimulia jinsi wanavyosumbuliwa na ndoto mbaya wakiwazia wapendwa wao wakioza chini ya uangalizi wake.
Baadhi yao walimtaja kama “jitu la kutisha” na kusema anastahili kuozea gerezani.
Aliyekuwa mke wake na pia mmiliki mwenza wa biashara hiyo, Carie Hallford, amekiri mashtaka yanayofanana na hayo na sasa anasubiri kuhukumiwa.
Mochari hiyo, Return to Nature, iliyoko Penrose, Colorado, iliwapa waombolezaji majivu ya bandia badala ya mabaki halisi ya wapendwa wao.
Waendesha mashtaka walisema miili 189 ilihifadhiwa vibaya ndani ya jengo hilo kwa kipindi cha miaka minne.
Mahakama ilijaa ndugu wa marehemu Ijumaa, wakimtaka jaji kutoa adhabu ya juu zaidi ya miaka 50 jela.
“Mimi ni binti ambaye mama yake alichukuliwa kama taka na kutupwa mahali pa kuoza pamoja na mamia ya wengine,” Kelly Mackeen aliambia mahakama.
“Nimevunjika moyo, na kila siku namwomba Mungu anipe neema.”

Miili hiyo ilipatikana ikiwa imepangwa kwa mafungu katika maeneo yasiyo na friji ndani ya mochari. Miongoni mwa waathiriwa walikuwa watoto na hata vijusi.
 “Ni imani yangu binafsi kwamba kila mmoja wetu, kila binadamu, kimsingi ana wema moyoni,” alisema Jaji Eric Bentley. “Lakini tunaishi katika dunia inayojaribu imani hiyo kila siku, na Bw Hallford, uhalifu wako unapima imani hiyo.”
Hallford, ambaye alikiri makosa akitumaini kupunguziwa adhabu, aliomba radhi kabla ya hukumu kutolewa. “Makosa yangu yataacha alama kwa kizazi kizima. Kila nilichofanya kilikuwa kibaya.”
Waendesha mashtaka walisema wanandoa hao walichochewa na tamaa ya fedha, licha ya kwamba walikuwa wakipata mapato ya kutosha kuweza kutunza miili ipasavyo.
Mochari hiyo, iliyo takriban kilomita 48 kusini mwa Colorado Springs, ilikuwa ikibobea kwa uhifadhi wa mili usiotumia kemikalo.
Biashara hiyo ilianza kuchunguzwa baada ya ripoti za uvundo mkali kutoka eneo hilo. Maafisa waligundua miili 115 mapema Oktoba mwaka jana. Hallford alishtakiwa kwa kujaribu kuficha “uhifadhi usiofaa wa mabaki ya binadamu.”