Habari

Hasira, kilio, maandamano yazuka Huruma baada ya polisi kuua mwanafunzi wa KMTC

Na STEVE OTIENO February 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KILICHOKUSUDIWA kuwa jioni ya kawaida Jumamosi katika eneo la Huruma, Kaunti ya Nairobi, kiligeuka jinamizi kwa Bi Caroline Akinyi baada ya bintiye, 21, Cheryl Adhiambo, kulengwa jichoni kwa risasi polisi walipokuwa wakimkimbiza mhalifu katika eneo jirani.

Bi Cheryl, mwanafunzi wa Mwaka wa Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Matibabu, KMTC, aliyetazamia kukamilisha mitihani yake hii leo, Jumatatu, aliaga dunia papo hapo ndani ya kioski ya mama yake ya kuuzia samaki kupigwa risasi.

Ufyatuaji risasi huo ulitumbukiza Huruma kwenye ghasia na machafuko yaliyoendelea usiku kucha hadi jana adhuhuri.

“Nilikuwa nimeenda kumtembelea mtoto wangu shuleni nilipopigiwa simu na kufahamishwa binti yangu ameuawa. Nimeacha binti yangu mikononi mwa serikali. Sitaki kujua jinsi atakavyosafirishwa nyumbani kwa mazishi, jinsi suala lake litakavyoendelea, au iwapo atapata haki. Nimeachia serikali,” alisema Bi Akinyi, akizungumzia uhusiano ulioimarishwa miaka mingi kupitia kazi na ndoto, hatima iliyoishia mahali pale pale mazungumzo hayo yalipofanyikia.

“Sasa mtoto wangu amefia sehemu ile ile tuliposhiriki mazungumzo hayo na kumbukumbu nzuri. Nilimpata tu akiwa amelala mochari alfajiri. Moyo wangu ulivunjika hata zaidi nilipoona damu yake ilipomwagikia mahali alipopigwa risasi,” alisema.

Kufuatia mkasa huo, hali ilizorota ghafla huku maduka yakiporwa na kuwalazimu wafanyabiashara kufunga mapema.

Samani iliyopangwa kwenye barabara ya Mathare iligeuzwa vizuizi vya barabarani huku maduka yakiporwa mavazi na chakula.

Edwin Masibo, aliyekuwa anaelekea nyumbani kupitia Kangundo Road mwendo wa saa mbili usiku alisimulia: “Tulikumbana na mamia ya vijana wakipora na kuwashambulia watu. Simu, vibeti na vitambulisho vilitwaliwa. Maduka yaliporwa na ghasia kutanda.”

Kufikia jana asubuhi, wanaharakati eneo hilo walimsindikiza Bi Akinyi katika kituo cha polisi cha Huruma kuandikisha taarifa (OB).

Jaribio lao la kwanza lilizuiwa lakini hatimaye walikubaliwa kuingia mwendo wa adhuhuri.

Nje ya kituo, vifusi vya matatu mbili zilishuhudia ghasia zilizofanyika Jumamosi usiku.

Viongozi wa jamii eneo hilo walisema mauaji ya Cherly yanamulika mkondo wa kina wa ghasia.

Msemaji wa Muungano wa Wakazi Mathare Alfred Ochieng, alikashifu ufyatuaji risasi huo akitaja kisa hicho kuwa utepetevu na ukiukaji sheria.

“Tunatoa makataa kwamba afisa wa polisi aliyempiga risasi Cheryl ni sharti akamatwe. Msichana huyo hakuwa na hatia,” alisema Bw Ochieng.

Mkazi mwingine aliyejitambulisha kama Okeyo alisema tukio hilo limewaathiri kisaikolojia.

“Kilichofanyika hapa kimetuathiri mno. Sisi ni watu wanaopaswa kulindwa, lakini badala ya kulinda maisha yetu, afisa wa polisi anayefahamika kwa kuwahangaisha vijana wetu, amefanya hivyo tena leo,” alisema.

Wakazi waliapa kuendelea kuandamana ikiwa haki haitofanyika.

“Tutaandamana hapa na kuonyesha upendo wetu kwa dada yetu Cheryl, mwanafunzi wa mwaka wa kwanza KMTC — mwanafunzi mwenzetu aliyeuawa ilhali alikuwa na maisha mbele yake.”

Mwanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu Hussein Khalid baadaye aliungana na wakazi katika Kituo cha Polisi cha Huruma akiitisha uwajibikaji kwa dharura.

Aliwakosoa polisi kwa kuzuia haki.

“Tumezungumza na mama na familia na tumejaribu kuingia Kituo cha Polisi cha Huruma kurekodi OB, na hadi sasa, polisi hawajaturuhusu ndani. Nambari ya OB ni haki ya kila mtu,” alisema.

Familia hatimaye iliruhusiwa kuingia kituoni kuandikisha taarifa yao.

Bw Khalid alikemea polisi kwa kuwakabili kikatili wakazi walipoandamana kulalamikia ufyatuaji risasi.

Alizitaka taasisi za uangalizi kuchukua hatua bila kuchelewa.

“Tunataka maafisa wa IPOA kushughulikia suala hili na kumkamata afisa husika leo. Hatutaki kulala kabla hajakamatwa ili yupate haki kwa Cheryl Adhiambo.”