Korti yapinga uundaji wa makundi kulinda kura
MAHAKAMA Kuu jijini Mombasa imewaachilia huru watu watatu waliokuwa wakikabiliwa na shtaka la mauaji, huku ikitoa onyo kali dhidi ya matumizi ya makundi ya ulinzi yasiyo rasmi (vigilante) katika kukabiliana na ghasia za uchaguzi wakati wa Uchaguzi Mkuu.
Katika hukumu iliyotolewa Februari 12 jijini Mombasa, mahakama iliwaachilia huru Rama Lenga Beja, Felix Mwangovi na James Mwamuye Charo kuhusiana na kifo cha Nicodemus Karima Shikahili.
Marehemu Nicodemus alikuwa mfuasi wa chama cha chungwa (ODM) na aliuawa usiku wa kuamkia uchaguzi wa Agosti 8, 2017 katika eneo la Kilifi Kusini.
Kesi hiyo ilitokana na juhudi za vijana wa eneo hilo waliokuwa wakiegemea upande wa ODM kuunda kikundi cha kushika doria kwa lengo la kuimarisha usalama kabla na siku ya uchaguzi.
Ushahidi uliowasilishwa mahakamani ulionyesha kuwa eneo la Kilifi Kusini lilishuhudia vurugu wakati wa uchaguzi wa mwaka 2013, yakiwemo matukio ya kuchoma nyumba na vifo ikiwemo polisi.
Kutokana na hali hiyo, takribani vijana 25 walijiweka kwa vikundi kushika doria katika maeneo yaliyotajwa kuwa hatari kufuatilia mienendo ya kutiliwa shaka na kutoa taarifa kwa maafisa wa polisi wa Kituo cha Polisi cha Chasimba pamoja na wazee wa vijiji.
Usiku wa Agosti 7, 2017, vijana 18 walitumwa kwa kutumia pikipiki sita kufuatilia hali ya usalama katika maeneo ya Banda la Salama, Mwarakaya, Kaoyeni na Kizingo.
Shikahili, aliyekuwa amesafiri kutoka Nairobi kushiriki katika uchaguzi, alijiunga na kikundi hicho.
Kwa mujibu wa ushahidi, mmoja wa waendesha pikipiki aliripoti kuona gari lililozua shaka na akaelekezwa kulifuatilia. Muda mfupi baadaye, taarifa zikasambaa kuwa alishambuliwa na pikipiki kuchukuliwa.
Wafuasi wengine wa kikundi hicho, akiwemo Shikahili, walielekea eneo hilo kutoa msaada lakini wakakumbana na umati wenye hasira.
Katika vurugu zilizofuatia, Shikahili aliachwa nyuma na baadaye kupatikana akiwa amejeruhiwa vibaya.
Ripoti ya uchunguzi wa maiti ilionyesha kuwa alikuwa na jeraha kubwa kichwani, majeraha ya kukatwa yaliyopenya hadi kwenye fuvu la kichwa, ubongo kuonekana wazi pamoja na mifupa kadhaa kuvunjika.
Alifariki kutokana na kuvuja damu nyingi kulikosababishwa na jeraha la kichwa.
Upande wa mashtaka ulidai kuwa washtakiwa, waliodaiwa kuhusishwa na shughuli za Chama cha Jubilee, walihusika katika mzozo huo uliosababisha kifo hicho.
Hata hivyo, mashahidi 13 wa upande wa mashtaka hawakutoa ushahidi wa moja kwa moja unaowaonyesha washtakiwa wakimshambulia marehemu.
Aidha, dereva wa pikipiki ambaye alidaiwa kufuatilia gari hilo na ambaye tukio lake lilichochea mtafaruku, hakufika kutoa ushahidi, jambo ambalo mahakama ililitaja kuwa pengo kubwa katika uchunguzi.
Katika uamuzi wake wa kuwaachilia huru, jaji alieleza kuwa upande wa mashtaka haukufaulu kuthibitisha bila shaka yoyote kwamba washtakiwa ndio waliosababisha majeraha yaliyompelekea marehemu kifo.
“Kwa hivyo, washtakiwa wote wameachiliwa huru,” Mahakama ilisema huku ikitambua kuwa kundi hilo lilianzishwa kutokana na hofu ya vurugu za hapo awali, ilionya kuwa kuundwa kwa makundi ya ulinzi yenye misingi ya kisiasa na yasiyo na usimamizi madhubuti kunaweza kuhatarisha usalama na utulivu wa jamii.
Mahakama ilielekeza vyombo vya usalama, tume ya uchaguzi na wadau wengine kushirikiana kuweka mifumo ya kisheria, jumuishi na iliyoratibiwa vizuri ya usalama wa kijamii kabla ya chaguzi zijazo.