Habari za Kitaifa

Serikali ya Kenya yamsaka raia wa Urusi aliyejirekodi akiwinda wanawake kimapenzi

Na FATUMA BARIKI February 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI imesema inamtafuta raia wa Urusi anayedaiwa kuvizia wanawake wa Kenya, kushiriki nao mapenzi na kutundika video kwenye kurasa zake.

Waziri wa Jinsia Hanna Wendot ametaka waathiriwa wa kisa hicho kutafuta huduma za ushauri nasaha na usaidizi wa kisheria kupitia nambari 1195.

Kisa cha raia huyo wa Urusi kiliibuka siku chache zilizopita wakati video nyingi zilipotapakaa mitandaoni zikionyesha mwanamume huyo akisimamisha wanawake tofauti tofauti na kuwaalika kwa miadi katika chumba chake cha kukodisha ambako inaaminika alirekodi wakila ufuska na kuzituma kwa watu wasiojulikana kujipatia umaarufu au kulipwa.

Ripoti zinasema kwamba Kenya sio taifa pekee ambako mwanamume huyo alifanya vitendo hivyo. Raia wa Ghana na Nigeria pia wamesikika mitandaoni wakilalamika kwamba mwanamume huyo alifanya hayo katika mataifa yao.

“Hili ni kosa kubwa la dhuluma za kijinsia kwa kutumia teknolojia kunyanyasa. Kama serikali, tunalichukulia kwa uzito mno na tutatumia mbinu zote kupata haki,” ikasema taarifa ya Waziri Wendot Jumatatu, Februari 16, 2026.

Aliongeza kwamba serikali inatumia ushirikiano wa kimataifa yakiwemo mashirika yanayolinda wanawake na watoto kuhakikisha kwamba mshukiwa anayetuhumiwa kuvunja sheria za Matumizi Mabaya ya Kompyuta na Makosa ya Mitandaoni anatiwa mbaroni.

“Kando na hayo, wizara itatilia mkazo sera za ulinzi mitandaoni na unyanyasaji wa kidijitali kulinda wanawake na watoto dhidi ya maovu ya kimwili na kwenye safu za mitandao,” ikaongeza taarifa.

Waziri huyo pia ametahadharisha Wakenya dhidi ya kusambaza video na picha hizo akisema zitaongeza madhara ya kisaikolojia kwa waathiriwa.