Iran yataka Amerika iwe wazi kuhusu faida za muafaka kabla ya kuketi kuzungumza
TEHRAN, Iran
IRAN sasa inapendekeza kuwa mazungumzo kati yake na Amerika, kuhusu mpango wake wa kinyuklia, yanafaa kuzalisha faida za kiuchumi kwa pande zote mbili, mwanadiplomasia mmoja wa nchi hiyo aliripotiwa kusema Jumapili.
Haya yanahiri siku chache kabla ya kuanza kwa mazungumzo kati ya nchi hizo mbili.
Iran na Amerika zilifufua mazungumzo mapema mwezi huu ili kumaliza mzozo ambao umedumu kwa karibu mwongo mmoja kuhusu mpango wa kinyuklia wa Iran na kuepusha makabiliano ya kijeshi.
Amerika imetuma chombo cha pili cha kubeba ndege karibu na Iran ishara kwamba inajiandaa kwa uwezekano kuchukua hatua za kijeshi dhidi ya nchi hiyo endapo mazungumzo hayatazaa matunda, afisa mmoja wa Amerika aliambia shirika la habari la Reuters.
Lakini Waziri wa Masuala ya Kigeni wa Amerika Marco Rubio, akihutubia kikao cha wanahabari mjini Bratislava, nchini Slovakia, alisema Rais Donald Trump ameweka wazi kwamba alikuwa amependelea kuwa mzozo huo utatuliwe kidiplomasia na kwa njia ya mazungumzo, huku (waziri huyo) akiweka wazi kuwa huenda hilo lisifanyike.
“Hamna aliyewahi kufaulu katika mazungumzo na Iran lakini tutajaribu,” Rubio akasema.
Iran imetisha kushambulia vituo vya Amerika katika Mashariki ya Kati endapo itashambuliwa na wanajeshi wa Amerika.
Hata hivyo, mnamo Jumapili ilitoa kauli iliyoashiria kuwa inasaka maridhiano.
“Ili makubaliano yaweze kudumu, ni muhimu kwa Amerika pia kufaidi katika nyanja zenye manufaa ya juu na haraka ya kiuchumi,” Naibu Mkurugenzi wa kitengo cha diplomasia ya kiuchumi katika Wizara ya Masuala ya Kigeni Hamid Ghanbari akasema, kulingana na Shirika la Habari la Far.
“Masilahi ya pamoja katika sekta ya mafuta na gesi, uwekezaji katika sekta ya madini na hata ununuzi wa ndege yataangaziwa katika mazungumzo hayo,” Ghanbari akasema, akiongeza kuwa mwafaka wa kinyuklia ya 2015 na mataifa yenye nguvu duniani hayakulinda masilahi ya kiuchumi ya Amerika.
Mnamo 2018, Tump aliiondoa Amerika kutoka kwa mwafaka huo ambao ulikuwa umelegeza vikwazo vilivyowekewa Iran.
Mnamo Ijumaa, duru ziliambia Reuters kwamba ujumbe mmoja wa Amerika ulioshirikisha mabalozi Steve Witkoff na Jared Kushner, utakutana na maafisa wa Iran jijini Geneva, Uswizi, Jumanne.
Mkutano huo ulithibitishwa na afisa wa ngazi ya juu katika serikali ya Iran.
“Steve Witkoff na Jared Kushner watasafriri, nadhani wanasafiri sasa hivi, kwa mikutano muhimu na tunasubiri kuona kitakachojiri,” Waziri Rubio akasema, bila kutoa maelezo zaidi.
Japo mazungumzo yaliyowezesha kufikiwa kwa makubaliano wa kinyulia ya 2015 yalishirikisha mataifa mengi, mazungumzo ya sasa yanashirikisha Iran na Amerika pekee huku Oman ikihudumu kama mpatanishi.
Waziri wa Masuala ya Kigeni wa Iran Abbas Araqchi Jumapili alisafiri kuelekea Geneza kushiriki katika mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja na Amerika.
Aidha, aliratibiwa kukutana na mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kusimamia mpango wa kinyulia (IAEA) na maafisa wengine, kulingana na taarifa iliyotolewa na wizara yake.
Naye Naibu Waziri wa Masuala ya Kigeni Majid Takht-Ravanchi aliashiria kwa Iran iko tayari kukomesha baadhi ya mipango yake ya utengenezaji wa zana za kinyuklia ili ilegezewe vikwazo.
“Sasa kazi ni kwa Amerika kuthibitisha kuwa wamejitolea kwa makubaliano kuhusu suala hili,” Takht-Ravanchi akawaambia wanahabari.