Museveni: Huwa sijilazimishi kwa wananchi, utendakazi wangu ndio unanipa mihula mingi
KAMPALA, UGANDA
RAIS wa Uganda Yoweri Museveni amewashauri viongozi wasiwe watu wa kujilazimisha kwa wapigakura na kukwama mamlakani bali waheshimu demokrasia na uamuzi wa raia.
Kiongozi huyo alisema viongozi wanastahili kuchaguliwa kwa haki na kutegemea uchapakazi wao badala ya kukesha wakiwachochea na kuwatia raia fitina ili washinde.
Museveni alisisitiza kuwa uongozi ambao unajikita katika kuwahangaisha na kuwatishia raia haumfikishi kiongozi mahala popote.
“Washawishi watu kwa kufanya mambo mazuri ambayo wanayaona na wanapenda badala ya fitina na kudhoofisha asasi ambazo zipo,” akasema Rais Museveni.
Museveni alikuwa akizungumza mnamo Jumanne katika Wilaya ya Kitgum wakati wa maadhimisho ya Siku ya St Janani Lawum.
Maadhimisho hayo pia yalihudhuriwa na mkewe Museveni, Janet ambye na Waziri wa Michezo na Elimu.
“Kosa la kwanza la Amin lilikuwa kujilazimisha kwetu. Alifikiria yeye ni nani? Viongozi hawafai kujilazimisha kwa raia,” akasema Museveni akionekana kukerwa.
“Bibilia na mikakati ya kisiasa inatuonyesha kuwa kuongea na watu ni bora kuliko kujilazimisha kwao ukisaka uongozi,” akaongeza.
Kiongozi huyo wa NRM pia aliwashukuru wapigakura wa kaskazini mwa Uganda kwa kumchagua kwenye uchaguzi mkuu wa Januari 15 ambapo alimbwaga mpinzani wake wa karibu Robert Kyangulanyi maarufu Bobi Wine.
Alisema amefurahishwa na mkengeuko wa kisiasa wa eneo hilo kwa sababu kwa miaka mingi, hawajakuwa wakiwachagua wawaniaji wa NRM.
“Hapa hamkuwa mkitupigia kura na kwa wakati mmoja tulikuwa tukipata asilimia 12 kisha ikaanza kupanda mnamo 2011. Hata hivyo, mmeona kazi yetu na mkaanza kutupigia kura,” akasema rais huyo.
Alisema kuchangamkiwa kwake debeni na wakazi wa eneo hilo kulitokana na serikali yake kuwekeza katika miradi ya miundomsingi, elimu na kuanzisha miradi kadhaa kwenye sekta ya kawi, maji na afya.
Alitaja kukamilishwa kwa ujenzi wa barabara ya Acholibur-Kitgum-Musingo ambayo alisema imefungua eneo hilo kiuchumi.
“Baada ya muda fulani wakazi wa hapa walianza kuamini kuwa Museveni na NRM ni wazuri. Nawashukuru kwa kunipigia kura kwa sababu niliwarai, nikachapa kazi na sikujilazimisha kwenu,” akasema Museveni.
Viongozi mbalimbali ambao waliandamana na Museveni katika ziara hiyo walimsifu na kusema kuwa NRM kushinda viti vingi vya uwakilishi eneo hilo kunadhibitisha kuwa kazi ya serikali sasa inaonekana.
Museveni pia alionya jamii ya Acholi na kuitaka ikome wizi wa mifugo akisema tabia hiyo imepitwa na wakati na watakaonyakwa watachukuliwa hatua kali kisheria na kushughulikiwa kama wahalifu.