Kibagendi akaidi agizo la Spika Wetangula licha ya kupigwa marufuku bungeni
MBUNGE wa Kitutu Chache Kusini Antony Kibagendi hajaonyesha kushtuka baada ya kupigwa marufuku kuhudhuria vikao vya Bunge kwa kile ambacho Spika Moses Wetangula alitaja kuwa matamshi yanayodhalilisha Bunge.
Akizungumza Jumanne, Februari 17, Wetang’ula alisema Kibagendi alitoa madai mazito katika mahojiano ya televisheni akidai kuwa Bunge limepigwa mnada na kwamba Spika pamoja na manaibu wake wameharibu taasisi hiyo.
Spika Wetangula alisema kauli hizo zilikuwa za kupotosha na zililenga kutia doa Bunge.
Kutokana na hilo, Kibagendi alizuiwa kuhudhuria vikao vyote vya Bunge, vikiwemo vya kamati, kuingia katika majengo ya Bunge na hata kufika ofisini kwake hadi atakapowasilisha barua ya kuomba msamaha iliyoandikwa ipasavyo kwa Karani wa Bunge ili ichunguzwe.
Kufikia wakati wa kuandika Makala haya, hakukuwa na ripoti kwamba aliandika barua hiyo.
Pia soma: https://taifaleo.nation.co.ke/habari/kibagendi-azimwa-kufika-majengo-ya-bunge/
Bw Kibagendi, ni baadhi ya wabunge waasi wa chama cha ODM wanaopinga serikali jumuishi – inayotokana na ushirikiano kati ya Rais William Ruto na kiongozi wa chama hicho marehemu Raila Odinga.
Kabla kufariki, Bw Odinga alikuwa akishirikiana sako kwa bako na Rais Ruto, katika kile alichokitetea kama mbinu kutuliza joto la kisiasa nchini hasa baada ya maandamano ya kizazi cha Gen Z 2024 na 2025.
Baadhi ya wabunge wa ODM wameonekana kupinga hadharani ushirikiano huo, wabunge hao wakijumuisha Kibagendi, seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Gavana wa Siaya James Orengo, kati ya wengineo.
Kwa sasa, ODM inaongozwa na kakaye mkubwa wa Raila Odinga, Dkt Oburu Odinga ambaye pia ni seneta wa Siaya.