Man City yatoa onyo kali kwa Arsenal
USHINDI wa 2-1 wa Manchester City dhidi ya Newcastle Jumamosi usiku, Februari 21, 2026 uliongeza shinikizo kwa vinara Arsenal kabla ya mechi yao na Tottenham usiku jana katika mbio za kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).
Mabao mawili ya Nico O’Reilly dakika ya 14 na 27 yaliiwezesha City kuvuna alama zote tatu.
Bao la kufutia machozi la wageni liliungwa na Lewis Hall dakika ya 22.
The Gunners walifufua matumaini ya City kuchukua ubingwa baada ya kutoka sare ya 2-2 na wavuta mkia Wolves katikati ya wiki jana.
Wachezaji wa City walionekana wakisherehekea baada ya firimbi ya mwisho, hii ikiwa ni kutokana na afueni pamoja na furaha kufuatia mechi hiyo ngumu Ugani Etihad.
Pep Guardiola amejenga upya kikosi chake cha City kilichoshinda mataji manne ya EPL mfululizo, hivyo maswali yanabaki kuhusu ikiwa wanaweza kuendeleza msururu wa matokeo mazuri katika mechi 10 zilizosalia.
Kwa ushindi huu, inaweza kuwa si rahisi sana, lakini jambo la msingi ni kwamba City wana kasi ya ushindi ambayo ni ya kutisha Arsenal.
Guardiola alifurahishwa sana na ushindi huo hivi kwamba, alitangaza kuwa wachezaji wake wanaweza kufurahia siku tatu za mapumziko na wanyweji vinywaji.
Pia soma: https://taifaleo.nation.co.ke/dimba/arsenal-waanza-kuporomoka/
“Nawaambia wachezaji: Jamani, tunachotakiwa kufanya ni kunywa caipirinhas na daiquiris nyingi katika siku hizi tatu [za mapumziko]!” alisema Guardiola.
“Furahieni maisha. Na baada ya hapo, fanyeni mazoezi matatu mazuri, na twende Leeds.”
Ushindi wa City unawaacha pointi mbili pekee nyuma ya Gunners, ambao walionyesha dalili za kuyumba walipoachilia uongozi wa mabao mawili na kutoka sare na Wolves.
“Uhusiano tulionao na mashabiki wetu ulikuwa bora zaidi msimu huu. Tulikuwa na hali nzuri zaidi na tunahitaji hali hizo kati ya sasa na mwisho wa msimu.”
Anaamini kuwa asilimia 70 ya kikosi chake cha sasa hakijawahi kupitia njia hii ya ubingwa, lakini bado kuna wengi ambao wamefanya hivyo, kama vile Ruben Dias na Rodri kwa kutaja wachache, na muhimu zaidi Guardiola mwenyewe.
Newcastle nao waliendelea kusalia nafasi ya 10 na alama 36 alama sawa na Sunderland walio nafasi ya 11.
Chelsea waliandikisha sare ya pili mtawalia EPL dhidi ya Burley (1-1) Ugani Stamford Bridge mnamo Jumamosi.
Aston Villa nao waliandikisha matokeo sawia na hayo dhidi ya Leeds United. West Ham United walitoka sare tasa dhidi ya Bournemouth nao Brighton wakainyoa Brentford 2-0 ugenini.