Akili MaliMakala

Pampu tamba ya kawi kuboresha kilimo hasa maeneo kame

February 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SEKTA ya kilimo nchini na bara la Afrika kwa jumla inazidi kukeketwa na athari za mabadiliko ya tabianchi, hususan ukame sawa na ulioshuhudiwa Januari 2026 katika zaidi ya kaunti 25. 

Ni changamoto inayohitaji wakulima, wafugaji na wadauhusika kutathmini ukumbatiaji wa teknolojia na bunifu za kisasa kuleta suluhu.

Teknolojia za kisasa, hasa wakati huu Kenya, Afrika na ulimwengu kwa jumla unakumbwa na athari za tabianchi itasaidia kuzitatua.

Eneo kame Kaunti ya Machakos lenye mfumo wa irrigation kuendeleza kilimo. Picha|Sammy Waweru

Rik Haanen, Afisa Mkuu Mtendaji wa Jacana Foundation, ni mmoja washirika wanaojituma kuibuka na bunifu kuangazia gapu hiyo.

Kwa miaka mingi amekuwa akifanya kazi kwa karibu na wajasiriamali barani Afrika. Ametembea Zambia, Msumbiji, Malawi, Tanzania na Ghana, ambako wengi wa wajasiriamali anaofanya nao kazi ni wakulima.

Wengi wao, anakiri changamoto kubwa inayoathiri mavuno na mapato ni maji. “Upungufu wa maji umekuwa tatizo kubwa,” Haanen anasema.

Rik Haanen, Afisa Mkuu Mtendaji wa Jacana Foundation akielezea kuhusu utendakazi wa pampu tamba ya sola. Picha|Sammy Waweru

Wakulima kuendelea kutegemea mvua, kunamaanisha miezi ya ukame uzalishaji hautakuwepo, ilhali mifumo ya umwagiliaji maji mashamba na mimea kwa kutumia mifereji (irrigation) wakati wa kiangazi inaweza kuongeza mavuno na mapato maradufu, ikiwa ni pamoja na kuimarisha usalama wa chakula.

Ipatayo miaka sita iliyopita, Jacana Foundation ilianza kuunda pampu ya sola kwa wakulima wa mashamba madogo.

“Lengo lilikuwa kuitengeneza iwe na uwezo wa kusambaza maji ya kutosha bila kuwa na bei ghali, na itumie nishati ya jua kwa kuwa nguvu za umeme vijijini ni haba,” Haanen anaelezea.

Seti nzima ya pampu tamba ya kawi kuboresha kilimo hasa maeneo kame. Picha|Sammy Waweru

Safari haikuwa rahisi; baadhi ya miundo iliharibika baada ya mwaka mmoja. Hata hivyo, baada ya majaribio kadhaa, walipata muundo imara na kuanza kuusambaza.

Mwanzoni, paneli ya sola ilikuwa ikiwekwa nje ya nyumba ya mkulima.  Lakini mkulima mmoja alilalamika kuwa hakuwa na imani ya kuiacha nje usiku kwa hofu ya kuibiwa. Hapo ndipo alipoibuka na ubunifu wa kipekee.

Pampu yenye paneli ikaundwa, inayotolewa nje na kuhifadhiwa ndani usiku.

Sola kuunda nguvu za kawi ili kusaidia pampu kusambaza maji shambani. Picha|Sammy Waweru

Siku iliyofuata, Haanen anadokeza kwamba mkulima huyo aligundua kwamba pampu ilikuwa ndogo na nyepesi kiasi cha kuibeba hadi shambani umbali wa kilomita moja.

“Kutoka hapo tulihakikisha mitambo tunayotengeneza ni tamba na inayoondolea mkulima hatari ya kuibiwa.”

Chini ya siku chache, wakulima wengine walivutiwa na suluhisho hilo linalopunguza wizi na kuruhusu umwagiliaji popote. Leo hii, karibu wakulima 800 wanatumia pampu hiyo, wengi wao wakiwa Zambia na wengine Msumbiji, Malawi, Tanzania na Ghana.

Rik Haanen, Afisa Mkuu Mtendaji wa Jacana Foundation wakati wa mahojiano na Akilimali akielezea alivyoibuka na pampu tamba ya sola kuendeleza kilimo. Picha|Sammy Waweru

Kulingana na Haanen, kuna wakulima wa mashamba madogo milioni 33 Afrika Kusini, na wengi wao hawajakumbatia mifumo ya kisasa ya irrigation.

Pampu tamba ya mbunifu huyo huja na paneli ya jua ya wati 160 inayokunjika na pampu ya kuzamishwa majini ya wati 100.

“Inaweza kupampu hadi lita 25,000 za maji kwa siku, hili likitegemea kiwango cha maji kwenye chanzo na mwanga wa jua,” Haanen akaambia Akilimali kwenye mahojiano ya kipekee.

Rik Haanen akiwekelea mgongoni baadhi ya vifaa vya pampu tamba ya sola. Picha|Sammy Waweru

Nchini Kenya, teknolojia hii inahamasishwa kupitia kampuni ya Maji Milele, chini ya Afisa Mkuu Mtendaji Marcel Schreurs.

“Tunatazamia itawafaa zaidi wakulima wa mashamba madogo,” Schreurs anasema. Pampu hiyo ilikuwa kati ya teknolojia na bunifu zilizotamba na kuvutia wakulima wakati wa maonyesho ya Africa Agri Expo yaliyofanyika ukumbi wa KICC, Nairobi Februari 11–12, 2026.

Maji yakitiririka kwenye pampu tamba ya sola. Picha|Sammy Waweru

Bei ya pampu moja ni Sh47,900 huku ya pampu mbili ikiwa Sh85,000.

Kimsingi, matumizi ya sola kuendeleza kilimo ni mojawapo ya mbinu kuangazia kero ya baa la njaa na usalama wa chakula haswa maeneo yanayoshuhudia ukame na kiangazi (ASAL).

Wakulima waliovutiwa na pampu tamba ya sola wakati wa maonyesho ya Africa Agri Expo yaliyofanyika ukumbi wa KICC, Nairobi Februari 11–12, 2026. Picha|Sammy Waweru