Kimataifa

Mamia waangamia Pakistan ikishambulia kundi la Taliban

Na MASHIRIKA February 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

PAKISTAN jana ilishambulia miji ya Kabul na Kandahar nchini Afghanistan na kutangaza vita dhidi ya uongozi wa Taliban.

Mashambulizi hayo yalithibitishwa na nchi zote mbili mnamo Ijumaa.

Wizara ya Ulinzi ya Pakistan imesema kuwa mzozo huo sasa huenda ukachochea mapambano makali kati ya majirani hao.

Hii ni mara ya kwanza Pakistan inatekeleza mashambulizi ya angani dhidi ya maeneo ya Taliban huku wakikwepa kulenga wapiganaji ambao wanawaunga mkono.
Nchi hizo mbili za Kiislamu zimekuwa na uhasama mkali kati yao.

Shambulizi hilo lililenga vituo vya kijeshi vya Taliban jijini Kabul, Kandahar na mkoa wa Paktia.

Pia iliripotiwa vita vikali kati ya mirengo hiyo miwili vilishamiri kwenye miji ya mipakani.

Taliban nayo ilisema kwamba ilikuwa ikiendelea kulipiza kisasi uvamizi wa Taliban.

Pande zote ziliripoti uharibifu mkubwa na maafa lakini hazikutoa takwimu.

“Tumekuwa na subira sana nao, kwa sasa tunatangaza kuwa tupo vitani dhidi ya Afghanistan,” akasema Waziri wa Ulinzi wa Pakistani Khawaja Muhammad Asif.

Pakistani imekuwa ikisema Afghanistan inawafadhili na kuwakinga wapiganaji ambao wamekuwa wakitekeleza uvamizi mipakani.

Taliban nao wamekanusha hilo na kusema suala la usalama wa Pakistani ni tatizo lao la kindani wala hawawezi kuliingilia.

Msemaji wa Taliban Zabihullah Mujahid alithibitisha kuwa wapiganaji wa Pakistani walitekeleza mashambulizi ya angani maeneo mbalimbali kama vile Kabul, Kandahar na Paktia lakini hakutoa ufafanuzi zaidi.

Kandahar ndio makao makuu ya Taliban na ndiyo jiji ambapo kiongozi wao wa kidini Haibatullah Akhundzada anaishi.

Mosharraf Zaidi, Msemaji wa Serikali ya Pakistani alisema kuwa walitekeleza mashambulizi hayo kama sehemu ya kulipiza kisasi uvamizi ambao umekuwa ukiendeshwa na Afghanistan.

Alidai kuwa waliwaua wapiganaji 133 wa Taliban na kuwajeruhi zaidi ya wengine 200.

Vituo 200 vya wapiganaji wa Taliban pia viliharibiwa na wakawashika mateka wanajeshi sita.

Mujahid, Msemaji wa Taliban alisema waliwaua wanajeshi 55 wa Pakistani na kutwaa maeneo yao tisa ya kivita.

Aliongeza kuwa wapiganaji wanane wa Taliban waliuawa, 11 wakajeruhiwa na raia 13 wakajeruhiwa mkoa wa Nangarhar.

Pakistani ina uwezo mkubwa wa kijeshi ikilinganishwa na Afghanistan.

Hata hivyo, Taliban nao ni wakali na hutumia mbinu ya guerrilla kuwakabili maadui.

Taliban inaonekana kukomaa na kutotikisika kutokana na miaka mingi ya kupigana na wanajeshi wa Amerika kabla ya kutwaa mamlaka mnamo 2021.