DRC kupanua vituo vya karantini vifo vikifika 291
SERIKALI ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DR Congo) imeanzisha karantini ya lazima ya siku 21 kwa watu wanaotoka katika maeneo yaliyoathiriwa na mlipuko wa ugonjwa wa Ebola, hatua inayolenga kuzuia kusambaa zaidi kwa virusi hivyo ndani na nje ya mipaka yake.
Hatua hiyo ilitangazwa Alhamisi huku idadi ya maambukizi na vifo ikiendelea kuongezeka nchini humo.
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya DR Congo, wasafiri wote wanaotoka katika maeneo yaliyoathirika watalazimika kukaa karantini kwa siku 21, kipindi kinacholingana na muda wa juu ambao dalili za Ebola zinaweza kujitokeza baada ya mtu kuambukizwa.
Serikali imesema hatua hiyo itasaidia kutambua mapema watu walioambukizwa na kuzuia maambukizi mapya.
Takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa tangu mlipuko huo utangazwe rasmi Mei 15 mwaka huu katika jimbo la Ituri, visa 1,118 vya Ebola vimethibitishwa huku watu 291 wakifariki dunia.
Hii ni sawa na kiwango cha vifo cha karibu asilimia 26, jambo linalozua wasiwasi mkubwa kwa mamlaka za afya na mashirika ya kimataifa.
Mlipuko huo unasababishwa na aina ya virusi vya Ebola Bundibugyo, ambayo ni nadra ikilinganishwa na aina nyingine za ugonjwa huo.
Wataalamu wa afya wanaeleza kuwa changamoto kubwa ni kwamba, hakuna chanjo au tiba maalumu iliyothibitishwa dhidi ya aina hiyo ya virusi, tofauti na baadhi ya milipuko ya Ebola iliyoshuhudiwa hapo awali.
Mbali na hatua za karantini, DR Congo tayari ilisimamisha safari za ndege kwenda na kutoka mji wa Bunia, kitovu cha mlipuko huo katika jimbo la Ituri.
Serikali ilisema ndege zilizowabeba wahudumi wa afya pekee ndizo zitaruhusiwa kufanya safari kwa kibali maalumu.
Mlipuko huo umeanza kuibua tahadhari katika mataifa jirani. Rwanda ilitangaza karantini ya lazima kwa wakazi wake wanaotoka DR Congo na kupiga marufuku wageni waliotembelea au kupitia nchini humo katika siku 30 zilizopita.
Nchi hiyo imesisitiza kuwa hadi sasa haijarekodi kisa chochote cha Ebola lakini imeimarisha ukaguzi mipakani na katika uwanja wa ndege wa Kigali.
Wakati huo huo, Ufaransa imethibitisha kisa chake cha kwanza cha Ebola kinachohusishwa na mlipuko wa DR Congo baada ya daktari aliyekuwa akihudumu mashariki mwa nchi hiyo kupatikana na virusi hivyo aliporejea Ulaya.
Tukio hilo limeongeza hofu ya kuenea kwa ugonjwa huo kimataifa.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limeonya kuwa mapambano dhidi ya Ebola yanatatizwa na migogoro ya kiusalama, ukosefu wa fedha na kutoaminiana kati ya jamii na wahudumu wa afya.
Wataalamu wanaonya kuwa bila ushirikiano wa kimataifa na hatua kali za afya ya umma, mlipuko huu unaweza kuwa mbaya zaidi kuwahi kushuhudiwa katika eneo hilo.