Kivuli cha Uhuru uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia
SWALI kubwa linaloibuka huku Uchaguzi Mkuu wa 2027 ukikaribia ni iwapo Rais mstaafu Uhuru Kenyatta ataathiri matokeo yake, huku akijitokeza waziwazi kumpinga tena Rais Rais William Ruto.
Katika juhudi zake za kusuka upinzani kwa maandalizi ya 2027, lengo lake likiwa kumzuia Rais Ruto kutetea kiti chake, Kenyatta anakutana na hali halisi huku akicheza karata zake chini ya maji.
Baadhi ya wakosoaji wanauliza nia ya Kenyatta, huku baadhi ya viongozi wa upinzani wakiwa na wasiwasi, wakisema kuwa huenda Rais mstaafu anamsaidia Rais Ruto.
Hii ni kwa kuwa Kenyatta amekutana na Rais Ruto mara mbili Desemba 2024 na Agosti 2025, huku upande wa serikali ukitumia mikutano hiyo kama ishara kwamba wanaweza kufanya kazi pamoja.
Hali hii imezua shaka kuhusu kile anachokusudia, huku maswali ya kisiasa yakijitokeza kuhusu ukweli wa ushirikiano wao na umoja wao kwa manufaa ya kisiasa.
Kitu kingine kilichozua maswali ni taarifa kwamba Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed, alijaribu kupatanisha Rais Ruto na Kenyatta. Inasemekana Ahmed alijaribu kufufua uhusiano kati ya wawili hao kwenye mkutano wa 39 wa Muungano wa wa Afrika mnamo Februari 15, 2026.
Washirika wa Rais Ruto walisema kuwa juhudi za upatanishi zililenga kutatua tofauti zao, na pia kwa maslahi ya siasa za ndani na za kikanda. Hata hivyo, hakuna taarifa rasmi kuhusu matokeo ya mkutano huo, lakini vyanzo vimearifu kuwa Ahmed aliwasihi wawili hao kuonyesha umoja kwa ajili ya utulivu wa Kenya na ushawishi wake katika eneo la Afrika Mashariki.
Kama ilivyotarajiwa, siasa za Kenyatta zimekuwa na changamoto nyingi na mashambulizi makali kutoka kwa wafuasi wa Rais Ruto na baadhi ya viongozi wa upinzani, lakini Kenyatta anaendelea kutumia ushawishi wake kama rais mstaafu, akiunganisha watu wenye nguvu kisiasa, wakiwemo viongozi kutoka vyama vya upinzani.Mwakilishi wa Wanawake kaunti ya Murang’a, Betty Maina, alitangaza kabla ya mkutano wa Desemba kati ya Rais Ruto na Rais Mstaafu Kenyatta kwamba wawili hao wataungana katika uchaguzi za 2027.
Alisema, “Bila hofu ya kukosea, natangaza kuwa wawili hao wanatarajia kushirikiana katika uchaguzi wa 2027 na hivi karibuni mtaona baadhi ya wafuasi wa Kenyatta wakiteuliwa serikalini.”
Muda mfupi baada ya hapo, viongozi wanaohusishwa na Kenyatta kama vile Mutahi Kagwe, Lee Kinyanjui na William Kabogo waliteuliwa mawaziri katika serikali ya Rais Ruto.
Hata hivyo, Kenyatta ameendelea kumuunga mkono aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Fred Matiang’i, kama mgombea wake anayependelea wa urais. Katika juhudi zake za kufanikisha mabadiliko ya kidemokrasia, Kenyatta anavutia kama rais mstaafu anayetoka familia yenye ushawishi mkubwa nchini na uwezo wa kukusanya fedha nyingi za kampeni. Kenyatta pia anatajwa kwa kufadhili vuguvugu la Linda Mwananchi linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino.
Pia amekuwa akijaribu kufufua Azimio la Umoja, ambalo alitumia kumsaidia Raila Odinga kugombea urais, kwa kumtaja Kalonzo Musyoka kama kiongozi wake.
Viongozi wa ODM wameelezea hofu yao kuhusu Kenyatta kuingilia siasa za chama chao, huku wakishutumu juhudi zake za kusambaratisha chama hicho baada ya kifo cha Raila Odinga.
Hata hivyo, huku Kenyatta akijizatiti na kuweka mikakati ya kisiasa, analazimika kujibu mashambulizi ya wafuasi wa Rais Ruto ambao wanamlaumu kwa kusuka mikakati ya kudhoofisha serikali ya sasa.
Kiongozi wa ODM, Oburu Oginga, alionya kuwa ni makosa kufanya mabadiliko ya uongozi wa muungano wa Azimio bila kushirikisha ODM, huku wakimlaumu Kenyatta kwa kudharau chama cha Raila.
Viongozi wengine wamesema kuwa ikiwa Kenyatta anatarajia kumsaidia Matiang’i kufika Ikulu, basi ni muhimu ajitokeze wazi wazi na kutoa mwelekeo wa kweli.
Kwa wakati huu, watu wanajiuliza ikiwa Kenyatta atakuwa kiongozi wa kweli wa upinzani, au anatumia nafasi hiyo kwa faida yake mwenyewe. Siasa za Kenyatta zinaonekana kuwa na mwelekeo wa kutaka kuhakikisha kuwa uongozi wake au wa urithi wake unaendelea hata baada ya 2027.
Hata hivyo, wapo wanaoamini kuwa Kenyatta akijitokeza wazi miongoni mwa viongozi wa upinzani, anaweza kuwa na manufaa kwa nchi kwa kusaidia kuleta umoja au kupigania maslahi ya wananchi. Lakini, licha ya hayo, bado hajatangaza wazi ni nani atafaidika kutoka na mwelekeo wake katika siasa za 2027.