Maoni

MAONI: Iran ilijichongea yenyewe kwa kutishia ‘kuifuta Israel kwenye ramani ya dunia’

Na DOUGLAS MUTUA March 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUZI nimeondoka Israel kukalipuka! Hadi kufikia jana, rafiki zangu waliojua kwamba nilizuru taifa hilo la kiyahudi wakiniandikia kuniuliza iwapo nimeondoka, au vita kati ya Israel, Amerika na Iran vimeanza nikiwa bado ningali huko.

Wanadhani ni muujiza kwamba niliondoka kabla.

Kujificha kwenye mahandaki, hasa ukiwa ugenini, lingekuwa jambo gumu sana. Hata hivyo, Waisraeli wenyewe wamezoea maisha hayo kwa kuwa nchi yao imekuwa katika hatari ya kuangamizwa na mataifa jirani tangu ilipoundwa mnamo mwaka 1948.

Hata kwenye uwanja wa ndege wa pekee nchini Israel, Ben Gurion, unaona maandishi yanayokuelekeza kwa kujificha iwapo lolote linatokea wakati wowote.

Uwepo wa mahandaki katika kiingilio cha nchi ni ishara tosha kwamba, ijapokuwa umekuja kwa heri, la shari linaweza kutokea, na umeandaliwa jinsi ya kupambana nalo.

Ajabu ni kwamba, Waisraeli wanajua wakati ambapo nchi yao inakaribia kuingia vitani. Marafiki zangu jijini Jerusalem waliniambia mara kwa mara nimalize shughuli zangu upesi ili niondoke, lau sivyo, huenda ningalikwama huko kwa muda mrefu.

Nilishuku kulikuwa na hatari nilipojulishwa na kampuni ya ndege ya Uholanzi kwamba ilifuta tiketi yangu ya kurejea Amerika.

Nilipouliza kwa nini, niliambiwa ndege zao hazingehudumu tena eneo hilo kwa sababu za kiusalama. Ilibidi nipitie Ufaransa.

Kuna maswali mengi sana ambayo watu wanaulizana kuhusu vita vinavyoendelea – hasa kutegemea upande ambao kila mmoja anaunga mkono – kuhusu ushirikiano wa Amerika na Israel katika kuipiga Iran.

Kwangu mimi, swali kuu zaidi ni: Kati ya Amerika na Israel, ni nchi gani inayoidhibiti nyingine? Unasalitika kujiuliza swali hilo unapotafakari jinsi ambavyo imekuwa rahisi kwa nchi hizo kushirikiana kuanzisha vita vikubwa na hatari dhidi ya Iran, ambayo kwa muda tukidhani haigusiki.

Swali hilo lilijibiwa na mmoja wa marafiki zangu, Wally, hata kabla sijaondoka Israel. Mcheshi huyo alitania kwamba jina Jerusalem limemeza Amerika (USA) kwa hivyo taifa hilo dogo ndilo linaloidhibiti Amerika. Ulikuwa utani, lakini Wally aliaminia kikweli.

Jambo ambalo watu wengi hawajui ni kwamba Israel imevumbua mambo mengi ya kiteknolojia, lakini baadhi, hasa ya kiusalama, yamekuwa yakifanyiwa kazi nchini Amerika. Ni kwa sababu hii ambapo nchi hizo hazina chaguo ila kushirikiana; Israel imekuwa ikinunua silaha Amerika.

Hata hivyo, biashara hiyo itafika mwisho. Inaripotiwa kwamba Israel imejenga viwanda vyake vya kuundia silaha, hivyo haitategemea ilizokuwa ikiuziwa na Amerika.

Bila shaka Amerika itaendelea kuipa Israel msaada wa kiulinzi, lakini, kinyume na awali ambapo msaada huo ulikuwa silaha, itaanza itaipa Israel pesa taslimu ili kujiundia silaha zake yenyewe.

Tafakari kuhusu Israel, hasa ikiongozwa na Benjamin Netanyahu, ikiunda silaha zake bila kumtegemea mtu! Itaunda vitu vya ajabu! Na itampiga itakayetaka, hasa ikishuku kwamba ana nia ya ‘kuifuta kwenye ramani ya dunia’ kama Waajemi (Iran) walivyotishia kabla ya kipigo wanachopata.

Je, Amerika na Israel zilifanya kosa kuishambulia Iran? La hasha! Hata mimi ningefanya hivyo. Unapoishi na jirani ambaye ameapa kukuangamiza akipata fursa, afua ni mbili: umwangamize kabla, au umpige na kumwacha dhaifu kiasi cha kutojifuta nzi!

Israel ina maadui wengi, baadhi yao hata hawatambui kwamba Israel ni nchi, lakini hakuna aliyeapa kwa kuaminia kwamba ataifuta kutoka kwenye ramani ya dunia ispokuwa Iran. Na si kutishia tu, Iran ilianzisha mchakato wa kuunda silaha za nyuklia.

Je, Israel ilipaswa kuketi kitako na kusubiri kuangamizwa? Hili ni suala la kutumia akili tu. Iran yenyewe ilikosa kutumia akili kwa kuwa haijawa na uhusiano mzuri na majirani zake wa kiarabu, tena wanahasimiana kwa misingi ya madhehebu ya dini – Shia (Iran) na Sunni (wengineo) – hivyo haina mtetezi.

Tayari kumtomasa simba ni hatari, lakini kumtomasa peke yako ni sawa na kujitia kitanzi. Kwa vyovyote vile utapapurwa au ufanywe kitafunio, tena utalengwa wewe pekee. Natumai Iran imejifunza na haitathubutu tena.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)