DPP aagiza mwendesha mashtaka afunguliwe mashtaka ya rushwa
AFISI ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) imeagiza mwendesha mashtaka mmoja anayehudumu katika Mahakama ya Makadara, Nairobi, afunguliwe mashtaka matatu ya kupokea hongo.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na ofisi ya DPP mnamo Machi 4, 2026, ilibainika kuwa stakabadhi zilizowasilishwa na EACC kuhusiana na madai ya rushwa dhidi ya Samuel Mugo Kiarie zilikuwa halali.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, baada ya tathmini huru ya ushahidi uliowasilishwa, DPP ilibaini kuwa kuna ushahidi wa kutosha na wa kuaminika wa kuendeleza mashtaka ya jinai dhidi ya mshukiwa.
“Baada ya tathmini huru ya ushahidi uliowasilishwa, DPP imeweka bayana kuwa kuna ushahidi wa kutosha na wa kuaminika dhidi ya Kiarie,” ilisoma sehemu ya taarifa hiyo.
Kutokana na hilo, DPP imeidhinisha mashtaka matatu ya kupokea rushwa kinyume cha Kifungu cha 6(1) pamoja na Kifungu cha 18 cha Sheria ya Kupambana na Rushwa, na kuagiza mshukiwa afikishwe mahakamani kujibu mashtaka hayo.
Aidha, DPP ilisisitiza kuwa hakuna mtu aliye juu ya sheria, bila kujali cheo, mamlaka au wadhifa wake serikalini.
“Tunarudia kwamba hakuna mtu aliye juu ya sheria. Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya afisa yeyote anayevuruga uadilifu wa mfumo wa haki ya jinai,” ilieleza taarifa hiyo.
ODPP ilisema itaendelea kutekeleza wajibu wake wa kikatiba kwa kuzingatia sheria, maslahi ya umma na utoaji wa haki.
Mshukiwa anatarajiwa kufikishwa katika mahakama kusikiza kesi hiyo ili kujibu mashtaka yanayomkabili.