Habari

Wito Wakenya wawe rada mvua ikitarajiwa kuendelea kunyesha na kusababisha mafuriko makubwa

Na BENSON MATHEKA March 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

IDARA ya Utabiri wa Hali ya Hewa Kenya imeonya kuhusu uwezekano wa mafuriko mapya katika maeneo ya jiji la Nairobi na vitongoji vyake, huku ikiwasihi wakazi kuwa waangalifu kutokana na hatari kubwa ya mafuriko ya ghafla.
Katika tahadhari iliyotolewa Jumamosi itakayodumu hadi Machi 9 saa moja jioni, idara hiyo ilisema mvua ya wastani hadi kubwa inatarajiwa kuendelea katika maeneo ya Nairobi , Kiambu na Kajiado.
Idara alionya kuwa hata mvua ya wastani inaweza kusababisha mafuriko ya ghafla na mtiririko wa maji juu ya ardhi, kutokana na hali ya udongo kujaa maji hasa katika maeneo ya mijini.
Katika kaunti ya Nairobi, mvua ya wastani hadi kubwa inatarajiwa kunyesha katika sehemu nyingi, ikitarajiwa kufikia kati ya milimita 20 na 60. Hata hivyo, baadhi ya maeneo yanaweza kupokea mvua kubwa ya zaidi ya milimita 80.
Maeneo yaliyotajwa kuwa katika hatari kubwa ni pamoja na Kibra, Dagoretti Kaskazini, Dagoretti Kusini, Embakasi, Makadara, Kamukunji, Roysambu, Westlands, Langata na baadhi ya maeneo ya Mathare, ambako mifumo mibovu ya mifereji ya maji inaweza kuongeza hatari ya mafuriko.
Katika Kajiado County, mvua kubwa pia zinatarajiwa katika baadhi ya maeneo, zikifikia kati ya milimita 40 na 100 hasa katika maeneo ya Kajiado North, West na Central.
Aidha, katika kaunti ya Kiambu, idara hiyo ilitabiri mvua ya zaidi ya milimita 80 katika baadhi ya maeneo kama Thika, Juja, Ruiru, Limuru, Kikuyu, Githunguri na Kabete, jambo linaloweza kusababisha maporomoko ya ardhi katika maeneo yenye miinuko.
Wakazi wa Kaunti ya Machakos pia wameonywa kuhusu mvua kubwa inayoweza kufikia milimita 80 katika maeneo kama Masinga, Mavoko, Kathiani, Machakos, Matungulu, Yatta na Kangundo, ambako mafuriko ya ghafla yanaweza kutokea katika maeneo ya mito.
Wakati huo huo, serikali imewasihi wananchi kuepuka kuendesha magari katika barabara zilizojaa maji, kujiepusha na maeneo ya miteremko mikali wakati wa mvua kubwa, na kuhakikisha maji ya kunywa yanachemshwa au kutibiwa kwa njia salama kabla ya kutumiwa.
Tahadhari hii imejiri muda mfupi baada ya Idara ya Polisi kuthibitisha imepata miili 13 zaidi kufikia Jumamosi mchana, na kufanya idadi ya vifo kutokana na mvua kubwa Ijumaa kufikia watu 23.