Mwashako achujwa kundi la wabunge wa Pwani Kindiki akimtaka ajitenge na upinzani
KUTANGAZA kwa mbunge wa Wundanyi Danson Mwashako kuwa atawania kiti cha ugavana Kaunti ya Taita Taveta na kudinda kuunga mkono serikali kwa awamu ya pili kunaonekana kumtia taabani kisiasa.
Msimamo wake wa kisiasa unaonekana kuwapa wengi tumbojoto, ikiwemo serikali kuu kwani anajitetea kwa kudhihirisha kuwa yeye ni mchapa kazi jambo ambalo limekuwa tishio kwa wawaniaji wengine.
Wiki hii, serikali kuu ikiongozwa na Naibu Rais Kithure Kindiki walizuru Kaunti ya Taita-Taveta ajenda kuu ikiwa kushawishi mbunge huyo ambaye ameonekena kuongoza wakazi wa Wundanyi kwa mihula miwili.
Hili limefanyika siku chache tu baada ya muungano wa wabunge kutoka kaunti sita za Pwani (CPG) kumng’atua mamlakani Bw Mwashako kama mwenyekiti wa muungano huo na kumchagua mwakilishi wa wanawake wa Kilifi Getrude Mbeyu kwa nafasi yake.
Uchaguzi huo ulionekena kama njia moja ya kumwadhibu mbunge huyo wa Wundanyi kwa kutounga mkono Rais William Ruto kwa awamu yake ya pili ya urais mwaka wa 2027.
Bw Mwashako, ambaye ni mbunge aliyechaguliwa kwa tiketi ya Wiper Patriotic Party ambaye alionekana kukataa kujiunga na chama cha UDA huku gavana wa sasa Andrew Mwadime ambaye alichukua uongozi kama mgombea huru akiingia katika mtego wa serikali na kujiunga na chama hicho.
Bw Kindiki katika ziara yake naye ameapa kutumia njia zote kumshawishi Bw Mwashako kutoshirikiana na upinzani.
“Wapi Danson Mwashako? Amehepa? Lazima aingie kwa serikali. Akiendelea kufuatana na watu wa DCP, tutamsafirisha,” Naibu wa rais Kindiki alionya Bw Mwashako.
Hivi karibuni, Bw Mwashako ambaye ameshikilia msimamo wake wa kutojiunga na serikali, amekuwa mstari wa mbele kukashifu uongozi wa Rais William Ruto akiwa na kundi la Linda Wananchi linaloongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na mbunge wa Embakasi kusini Babu Owino.
Katika mahojiano na wanahabari baada ya ziara ya Bw Kindiki Kaunti ya Taita-Taveta mapema wiki hii, Bw Mwashako alikashifu serikali kwa kuwahadaa wakazi kwa kuzindua miradi miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
“Kama ni haki yetu kujengewa barababra ya Voi kwenda Sagalla mbona wanaijenga sasa na hawakuianza mwaka jana kama walijua kwamba watu wa eneo hili ni wa muhimu? Haimaanishi kwamba kama mimi siko katika chama tawala, tuwapokonye wakazi wa Taita-Taveta miradi ya barabara, na kama watafanya hivyo, hawastahili kuwa katika uongozi kwani hawastahili kushikilia maendeleo eti kwa sababu hatuko nao,” alisema Bw Mwashako.
Hata hivyo, wachanganuzi wanamuonya Bw Mwashako kutojiunga na chama cha UDA iwapo anataka azma yake kuwa gavana itimie kwani serikali imekuwa na njama nyingi na Bw Mwadime ambazo Bw Mwashako amekuwa akizipinga.
“Bw Mwashako akikubali kuingia UDA atapambana na Bw Mwadime kwa mchujo ambaye amekuwa kipenzi cha serikali na kama njia ya kumwadhibu, watamnyima cheti dakika ya mwisho wakati hawezi kuhamia chama kingine,” alisema Bw Elijah Mwarondo, mkazi wa Wundanyi.
Mbunge huyo wa Wundanyi ameonekana mmoja wa viongozi ambao wako na nafasi kubwa ya kuchukua uongozi wa Kaunti hiyo mwaka wa 2027 kutokana na sifa za miradi aliyotekeleza katika eneobunge la Wundanyi kwa mihula miwili iliyopita.
Bw Mwashako hata hivyo, anatarajiwa kupata upinzani mkali kutoka kwa Seneta wa sasa Jones Mwaruma, Bw Mwadime, aliyekuwa Gavana wa kwanza Bw John Mruttu na mwenzake Bw Granton Samboja, pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Halmashauri ya Bandari nchini (KPA) John Mwangemi.
Hadi sasa, hakuna mwanamke ambaye ametangaza nia ya kuwania kiti cha ugavana katika Kaunti ya Taita Taveta, huku wagombea wote waliotangaza nia yao wakiwa ni wanaume.
Hata hivyo, kunasubiriwa iwapo wagombeaji hao watatii pendekezo la wazee kutoka Kaunti hiyo kuwapiga msasa kabla ya kuingia debeni.
Hivi majuzi, viongozi na wazee kutoka maeneo bunge ya Mwatate, Wundanyi, Voi na Taveta wamekuwa wakijadiliana jinsi ya kutoa viongozi mwaka ujao ambao watatimiza mahitaji yao.
Tangu kuanzishwa kwa ugatuzi, Kaunti ya Taita Taveta imekuwa na laana ya ‘Wantam’ kwani imeongozwa na magavana watatu: Mhandisi Mruttu (2013–2017), Bw Samboja (2017–2022), na Gavana wa sasa Bw Mwadime.
Kiongozi wa muungano wa wazee hao Bw Thomas Mwadeghu amesema ijapo kisheria na kikatiba kila mmoja ana haki ya kugombea kiti chochote cha siasa, muhula huu wa kisiasa utakuwa tofauti kwani wakazi wa eneo hilo wamehadaiwa kwa muda na viongozi waliotangulia.
“Viongozi kutoka miungano mbalimbali eneo la Taita na Taveta wanaungana kutoa mwelekeo wa kisiasa na licha ya wagombeaji kutokea wengi, tunatarajia kufanya mchujo kulingana na matakwa ya wakazi,” alisema Bw Mwadeghu.