Jamvi La Siasa

Ruto hawezi bei yangu na siwezi kukubali kununuliwa, aapa Natembeya

Na BENSON MATHEKA March 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Gavana wa Kaunti ya Trans Nzoia George Natembeya amepuuza madai kwamba anaweza kushawishiwa au “kununuliwa” kisiasa na Rais William Ruto kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

Akizungumza katika mahojiano na kituo cha televisheni cha humu nchini usiku wa Jumatano, Natembeya alisisitiza kuwa hatawahi kuwasaliti Wakenya kwa manufaa yake binafsi.

Gavana  huyo alisema hana mahitaji ya kibinafsi yanayoweza kumlazimisha kukubali vishawishi vya kisiasa, akiongeza kuwa viongozi wanaouza misingi yao kwa pesa huishia kuisaliti imani ya wananchi.

“Ruto hawezi kuninunua. Atanipa nini ambacho ninahitaji sana?” Natembeya alihoji.

Gavana huyo alisema ana uwezo wa kifedha wa kushughulikia majukumu yake ya kibinafsi bila kutegemea upendeleo wa kisiasa.

“Ikiwa ni kulipa karo ya watoto wangu, nalipa. Nina mshahara na pensheni. Na kama ni suala la chakula, mtu mmoja anahitaji kiasi gani?” alisema.

Natembeya pia alihoji mantiki ya viongozi kukubali vishawishi kwa gharama ya maslahi ya taifa. Alikosoa kile alichokiita utamaduni ambapo baadhi ya viongozi hushawishiwa kirahisi na pesa na kuacha misimamo yao ya kisiasa.

“Wazo hili la kununuliwa kama binadamu, unanunuliwa kisha unaisaliti nchi nzima, ni jambo baya sana,” alisema.

Alisisitiza kuwa ataendelea kusimama kidete kutetea maslahi ya Wakenya bila kujali shinikizo za kisiasa.

“Hakuna mtu atakayeninunua kamwe. Sitawasaliti Wakenya kwa sababu mtu ananipa kitu fulani,” alisema.

Natembeya aliwataka viongozi wenzake kupinga vishawishi vya kisiasa, akionya kuwa mipango kama hiyo mara nyingi hufichuka baadaye.

“Tusikubali kununuliwa. Ukishanunuliwa, hatimaye itajulikana kuwa ulinunuliwa,” alisema.

Katika siku za hivi karibuni, Natembeya ameibuka kama sauti yenye ushawishi katika siasa huku mirengo ya kisiasa ikianza kujipanga kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Bw Natembeya amepinga azma ya urais ya kiongozi wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) Rigathi Gachagua akisema hata kama mahakama itamruhusu kugombea katika uchaguzi wa 2027, hatamuunga mkono.

Licha ya wawili hao kuwa katika muungano wa upinzani, Natembeya alisema anaamini kuwa urais unafaa kuzunguka kati ya maeneo tofauti ya nchi.

“La, kwa sababu ninaamini urais unafaa kuzunguka. Jamii ya Mlima Kenya imekuwa nao kwa takriban miaka 43, karibu miaka thelathini na kitu jamii moja( ikitoa  rais). Na ukienda huko, hakuna tofauti kubwa… kama watu wa Kikendu Murang’a na wale wa Kabuchai, maisha ni yale yale. Wao wamepata rais sisi hatujapata, lakini maisha yetu ni sawa tu,” alisema katika mahojiano hayo.