LUGHA: Makosa ya kukanusha sentensi bila kuzingatia viambishi vya ngeli husika
UTUNGAJI wa sentensi sahihi za Kiswahili huzingatia ngeli. Ngeli ni kundi la nomino zenye sifa sawa kiupatanishi kisarufi.
Hata ingawa wapo wanafunzi wengi wanaoweza kutunga sentensi sahihi wakizingatia viambishi sahihi vya upatanisho wa kisarufi, wapo baadhi yao wenye changamoto ya kusahau au kuvidondosha viambishi hivyo wanapokanusha sentensi.
Kwa sababu hiyo, sentensi wanazokanusha hukosa kuwa sahihi.
Aghalabu utapata sentensi kama vile: Madereva wale waliyaegesha magari yao uwanjani.
Maseremala hawa walivitengeneza viti ishirini na vitano. Mkulima huyo ataipanda miche mingi shambani mwake.
Sentensi hizi aghalabu hukanushwa ifuatavyo: *Madereva wale hawakuegesha magari yao uwanjani.
*Maseremala hawa hawakutengeneza viti ishirini na vitano. *Mkulima huyo hatapanda miche mingi shambani mwake.
Sentensi hizo zimekanushwa bila kuzingatia viambishi ngeli: ya-, vi- na -i- mtawalia.
Mwandishi amevidondosha viambishi hivi katika sentensi. Ili kuzisahihisha sentensi hizi, tunafaa kusema: Madereva wale hawakuyaegesha magari yao uwanjani.
Maseremala hawa hawakuvitengeneza viti ishirini na vitano. Mkulima huyo hataipanda miche mingi shambani mwake.
Ili kukabili changamoto hii, mwanafunzi anafaa aisome kila sentensi kwa makini kabla ya kuikanusha na atambue kiambishi ngeli kilichotumiwa katika sentensi anayokanusha.
Mwanafunzi aihariri kila sentensi aliyokanusha ili kuhakikisha ni sahihi. Mwanafunzi afanye mazoezi ya kukanusha sentensi za namna hii akizingatia viambishi vya upatanisho wa kisarufi.