Makala

Vijana wataka mageuzi katika uongozi wa jiji la Nairobi

Na WINNIE ONYANDO March 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

VIJANA katika eneo la Riruta Satellite jijini Nairobi wameeleza hitaji la dharura la kubadilishwa kwa mfumo wa uongozi wa jiji ili kukabiliana na changamoto sugu zinazowakumba wakazi.

Haya yaliibuka wakati wa kongamano la kwanza la kushirikisha umma lililoandaliwa na Mtetezi, vuguvugu la kutetea haki za binadamu, mnamo Machi 21, 2026.

Kwenye kongamano hilo, vijana walizungumzia kwa uwazi matatizo yanayowakabili kila siku yakiwemo mafuriko yanayoharibu makazi na biashara, majengo yasiyo salama, msongamano wa magari, ukosefu wa ajira na shinikizo kwa huduma muhimu.

“Changamoto hizi zinaonyesha kuna kasoro katika mfumo wa uongozi wa jiji,” alisema mmoja wa washiriki.

Takriban asilimia 68 ya waliohudhuria waliunga mkono pendekezo la kuifanya Nairobi kuwa jiji maalum la kimetropolitan, wakisema hatua hiyo itaimarisha mipango ya maendeleo, usimamizi na uratibu wa huduma.

“Muundo huu utawezesha utekelezaji bora wa sheria na kuboresha miundombinu,” aliongeza mshiriki mwingine.

Hata hivyo, asilimia 21 walipendekeza mfumo mseto ambapo gavana angeendelea kuchaguliwa lakini serikali ya kitaifa ichukue jukumu kubwa katika masuala ya miundombinu na mipango mikubwa.

Wengine asilimia 10 walitaka mfumo wa sasa wa kaunti ubaki, wakihofia ongezeko la urasimu na kupungua kwa uwajibikaji kwa wananchi.

Washiriki wengi walilalamikia siasa kuingilia uongozi wa jiji, wakisema mizozo kati ya viongozi huathiri utoaji wa huduma.

“Tunataka uongozi unaozingatia taaluma, si siasa kila wakati,” alisema Francis Awino, kiongozi wa vuguvugu hilo.

Licha ya tofauti zao, washiriki walikubaliana kuhusu umuhimu wa kuimarisha utekelezaji wa sheria hasa katika sekta ya ujenzi, kuboresha mipango ya miji, kupunguza msongamano wa magari na kuhakikisha miradi inaendelea hata baada ya uchaguzi.