Kesi nyingine yawasilishwa kupinga ushindi wa Atwoli
KESI nyingine imewasilishwa katika mahakamani kupinga kuchaguliwa tena kwa Francis Atwoli kama Katibu Mkuu wa COTU-K.
Katika ombi hilo lililowasilishwa kwa dharura, mwanaharakati Francis Awino anataka kusimamishwa kwa utekelezaji wa matokeo ya uchaguzi huo, ikiwa ni pamoja na kutambuliwa kwa Francis Atwoli kama Katibu Mkuu wa COTU.
Mwanaharakati huyo chini ya vuguvugu Mtetezi, amepinga vikali mchakato wa uchaguzi akidai kuwa ulikiuka sheria na kukosa uwazi.
“Kukosa kutoa taarifa muhimu ni ukiukaji wa Katiba na kunanyima wafanyakazi haki ya kushiriki kikamilifu katika uongozi wa vyama vyao,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Kupitia kesi hiyo, wanataka mahakama itangaze uchaguzi huo kuwa ulikiuka katiba, izuie kutambuliwa kwa viongozi waliochaguliwa na iamuru kufanyika kwa uchaguzi mpya ulio wazi, huru na unaofuata sheria.
Haya yanajiri siku chache baada ya walalamishi wawili, Fazul Mahamed na taasisi ya Institute for Democratic Governance, kuwaislisha kesi mahakamani wakidai kuwa kura hiyo ilifanyika mapema kabla ya muda unaoruhusiwa kisheria katika mzunguko wa uchaguzi wa vyama vya wafanyakazi.
Katika kesi iliyowasilishwa katika Mahakama ya Ajira na Leba jijini Nairobi, walalamishi walitaka mahakama ibatilishe matokeo ya uchaguzi uliofanyika Machi 14 wakati wa mkutano wa wajumbe wa baraza tawala la COTU uliofanyika Kisumu.